CHUO cha Maendeleo ya Ujuzi, Ufundi na Viwanda (Furahika Education) la Jijini Dar es salaam kimetangaza nafasi za masomo ya ufundi bure kwa vijana wapatao 200 kwa kipindi cha Mwaka wa fedha wa 2022. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari leo tarehe 12 Mei, 2022, Mkuu wa chuo hicho, David Msuya, ameeleza kuwa chuo hicho kupitia wafadhili wake kitagharamia masomo ya ufundi kwa vijana 200 watakaoomba kujiunga nacho na kwamba wanachuo watatakiwa kuja na vifaa kwa ajiri ya kujifunzia.
Msuya alieleza kuwa chuo hicho kinachomilikiwa na taasisi ya elimu ya Furahika kimeamua kupitia wafadhili hao kusaidia vijana ili waweze kujiajiri wenyewe ama kuweza kuajiriwa maeneo mbalimbali.
Alitaja mafunzo yatakayotolewa na chuo hicho kuwa ni Compyuta na unesi na kwamba mwisho wa maombi ni Mei 16 , 2022 ambapo masomo yataanza Mei 18, 2022 na walengwa ni vijana waliyomaliza darasa la saba ambao hawakuchaguliwa kuendelea na shule sambamba na wa kidato cha nne.
Hata hivyo, mwenyekiti wa taasisi hiyo, Mohamed Ngweje amesema lengo la chuo hicho ni kuunga mkono jitihada za serikali za kupambana na tatizo la ajira kwa vijana na hivyo kukabiliana na umasikini uliyopo nchini.
Ngwenje ameeleza kuwa vijana hao 200 wamelipiwa gharama hizo na wafadhili na kwamba zoezi hilo ni la kila mwaka ambapo itasaidia kupunguza pia lindi la vijana wanaokaa vijiweni kwa kukosa shughuli ya kufanya.
“Vijana hawa watatakiwa kuja chuoni na vifaa vitakavyohitajika kwa ajiri ya kujifunzia tu, hakuna ngharama yoyote kwa kozi atakayosoma kwa mwaka mzima, hii ni fursa ambayo watanzania tunatakiwa kuichangamkia,” amesema Ngwenje.
Aidha, ametoa wito kwa wazazi na walezi wenye watoto ambao hawakupata nafasi ya kuchaguliwa aidha kuingia sekondari ama kidato cha nne kuwapeleka kujipatia ujuzi huo ambao utakuwa mkombozi kwa vijana wao katika maisha yao.
Leave a comment