MKAZI wa kijiji cha Musimi kata ya Sepuka wilayani Ikungi, Mkoa wa Singida, Ramadhani Mnyambi ‘Tandika’ (47) ambaye ni fundi madaraja amenusurika kufa baada ya kusombwa na maji ya mto umbali wa mita 30 akaokolewa na wenzake kwa kuvutwa na kamba. Anaripoti Mwandishi Wetu, Singida … (endelea).
Habari zilizopatikana juzi kutoka eneo la tukio, zinasema Mnyambi alisombwa na maji ya mto kutokana na ubishi wake akiwa amelewa, alipoambiwa aingie mtoni apime kina cha maji kwa mti na avue viatu, lakini alikataa.
Zilisema Mnyambi aliingia mtoni na viatu bila mti, viatu vikaingiwa maji akaangushwa yakamsomba kwa kasi hadi kwenye kona akakumbana na mti akaushika.
Wenzake walichukua kamba wakamkimbilia wakamtupia kamba wakamvuta nje ya mto wakamchangia Sh 5,000 za pole kwa kunusurika.
Katika mahojiano na mwandishi wa habari hii, Mnyambi alisema mvua kubwa ilionyesha Jumamosi jioni ilipokoma, akiwa na wenzake kwenye gari la kazi, alitumwa na wenzake kupima kina cha mto, lakini alipoingia alishituka maji yanamzidi nguvu na kumsomba lakini wenzake wakamwokoa.
Ilielezwa kuwa baada ya tukio hilo, daraja hilo linalojengwa na kampuni ya Lupila ya Sumbawanga na mto huo sasa vyote vitaitwa Tandika, kama kumbukumbu ya fundi mwenzao aliyenusurika kufa wakijenga daraja hilo.
Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi Singida kupitia Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini (TARURA) imeanza kujenga daraja kukarabati barabara za vijijini na kutengeneza zingine mpya hasa zinazounganisha kata, ili kurahisisha mawasiliano.
Ujenzi wa barabara hizo, sasa zinakwenda polepole kutokana na sehemu nyingi kutopitika kutokana na mvua kunyesha mfululizo tangu mwishoni mwa Desemba mwaka jana, hadi sasa, hivyo vifaa vya ujenzi kushindwa kufikishwa kwa muda unaotakiwa hivyo kazi hiyo kuwa ngumu.
Leave a comment