MAMLAKA ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) imefanikiwa kumuua fisi aliyeua watu wawili na kujeruhi watano katika Wilaya ya Lindi Vijijini Mkoani Lindi. Anaripoti Christina Haule, Morogoro … (endelea).
Kamanda wa Uhifadhi wa Kanda ya Kusini Mashariki, Abraham S. Jullu alisema mnamo tarehe 11 Mei, 2023 majira ya Saa kumi na mbili asubuhi Ofisi yake ilipokea simu kutoka kwa Mtendaji wa Kata ya Milola akitoa taarifa kuwa fisi amejeruhi watu watatu (3) katika Kijiji Cha Rutamba, watu wawili (2) Kijiji Cha Ng’apa na kusababisha vifo vya watu wawili (2).
Amewataja waliojeruhiwa na fisi huyo kuwa ni Suleman Mtambo, Hadija Said, Alpha Ibrahimu, Maria Sabuni na mwingine aliyetambulika Kwa jina moja (Steven) ambao wote walipelekwa Hospitali ya Sokoine Mkoani Lindi huku waliofariki walitambulika Kuwa ni Abilahi Pokosoi (50), na Saidi Makolela (75) ambapo fisi huyo aliawa majira ya mchana baada ya kupatikana.
Aidha, Kamanda Jullu amesema taratibu za kuwasaka fisi wengine katika maeneo mbalimbali ikiwemo Milola na Vijiji vya Wilaya ya Ruangwa zinaendelea na kuona namna bora ya kuwahamisha na kuwapeleka maeneo ya hifadhi.
Hata hivyo, TAWA inatoa pole kwa wahanga wa tukio hili na inatoa rai kwa wananchi wote kutoa taarifa mapema pale wanapowaona Wanyamapori Wakali na Waharibifu katika maeneo yao ili kuwawezesha Askari kuchukua hatua za kuwadhibiti mapema kabla hawajasababisha madhara kwa maisha ya watu na mali zao.
Vilevile, wananchi wanasisitizwa kuchukua tahadhari ikiwemo kuepuka kutembea nyakati za alfajiri na usiku, na kutofanya shughuli za kibinadamu kama vile kilimo na ufugaji pembezoni mwa hifadhi na maeneo ya mapito (Shoroba) ya wanyamapori.
Leave a comment