SERIKALI ya Tanzania, imeagiza kampuni ya uchimbaji madini ya Tembo Nickel Corporation Ltd, kufanya upya tathimini ya fidia kwa wananchi wanaozunguka Mgodi wa Nickel wa Kabanga, ulioko Ngara mkoani Kagera. Anaripoti Mwandishi wetu, Dodoma…(endelea).
Maagizo hayo yametolewa leo Jumanne tarehe 27 Aprili 2021, na Naibu Waziri wa Madini, Prof. Shukrani Manya wakati akijibu swali la Mbunge wa Ngara (CCM), Ndaisaba Ruhoro, bungeni jijini Dodoma.
Katika swali lake, Ndaisaba aliihoji serikali akisema “kwa vile kuna tahimini ilifanyika hapo awali kwa ajili ya kutoa fidia kwa wananchi wanaozunguka mgodi huu, ambapo ni ya muda mrefu na ilipoteza uhalali. Je, serikali ina mpango gani kurudia kufanya tathmini ili wananchi waweze kupata fidia?”
Akijibu swali hilo, Prof. Manya amesema, tathimini iliyofanyika awali imepoteza uhalali kwa mujibu wa sheria, na kuiagiza Kampuni ya Tembo Nickel kufanya tathmini upya kwa ajili ya kulipa fidia, ili waanze mradi wao.
“Kuhusu tahimini, ni kweli ilifanyika miaka ya nyuma na kwa mujibu wa sheria ikipita miezi sita inaonekana haifai na hivyo inatakiwa kurudiwa, katika miradi yote ya uchimbaji mkubwa hakuna ulioanza bila kufanya tahimini na wananchi kulipwa malipo stahiki,” amesema Prof. Manya na kuongeza:
“Na tunaelekeza makampuni ya wachimbaji wafanye zoezi hilo kabla ya kuanza kuchimba. Katika hili, tutawaelekeza Tembo Nickel warudie kufanya tahimini ili wafanye fidia na hatimaye mradi uweze kuanza.”
Kampuni ya Tembo Nickel ilianzishwa baada ya Kampuni ya LZ Nickel ya nchini Uingereza kuingia ubia na Serikali ya Tanzania tarehe 19 Januari 2021, wa uchimbaji madini ya Nickel katika eneo la Kabanga.
Leave a comment