TUME ya Taifa ya Ushindani (FCC) imeleza kuwa haihusiki na kucheleshwa kwa mfumo wa mabadiliko wa uendeshaji wa klabu ya Simba bali kuchelewa huko kunatokana na wahusika wa klabu hiyo kuwa na mwitiko hafifu katika kuwasilisha nyaraka mbele ya Tume hiyo. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Hivi karibuni Mwenyekiti wa bodi ya wakurugenzi wa klabu ya Simba, Mohammed Dewji alisema kuwa mchakato wa mabadiliko wa klabu hiyo umekwama FCC kutokana na kutowapa mrejesho.
Katika taarifa yao walioitoa hii leo tarehe 19 Novemba, 2020, FCC imeeleza kuwa waliamua kusimamisha mchakato huo ili kufanya uchunguzi wa kwanini hawakuwasilisha taarifa ya muungano kati ya klabu ya Simba na Simba Sports Club Company Limited jambo ambalo ni kinyume na kifungu cha 11 (2) cha kanuni ya ushindani.
Aidha pia FCC ilitaka maelezo na ufafanuzi kwanini klabu hiyo imefanya uteuzi wa mtendaji mkuu kabla ya uwekezaji kufanyika na pia kujua kiasi halali cha fedha anachopaswa kuweka mwekezaji Mohammed Dewji ili kuondoa mkanganyiko kati ya kiasi cha pesa kilichopo kwenye mkataba wa makubaliano na kile kinachotajwa kwenye vyombo vya habari.
Michakato hii yote ni kuifanya klabu hiyo kuelekea kwenye mfumo wa mabadiliko ya uwendeshaji kutoka kwa wanachama mpaka kwenye mfumo wa hisa.
Tayari mfanyabiashara Dewji ameshashinda zabuni ya ununuaji wa hisa asilimia 49 ambapo zinathamani ya Sh. 20 bilioni, huku hisa asilimia 51 zitauzwa kwa wanachama wa klabu hiyo.
Leave a comment