ALIYEKUWA Rais wa Chama Cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), Fatma Karume ameishauri uundwaji wa Mahakama maalum itakayochunguza vifo vinavyotokea katika mazingira yenye utata. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Fatma ametoa wito huo leo tarehe 11 Machi 2023 katika kongamano la kukusanya maoni ya wadau juu ya uboreshaji taasisi za haki jinai, lililoandaliwa na TLS na kufanyika jijini Dar es Salaam.
Mtetezi huyo wa haki za binadamu amesema kuwa, mahakama hiyo itasaidia Serikali kulinda maisha ya wananchi wake.
“Serikali na mfumo wa haki jinai haithamini maisha ya watu, tuseme Ulaya bila kujulikana sababu ya kifo changu kuna mahakama itaanza kushughulikia kujua nimefariki kutokana na sababu za asili au kuna kitu kingine,” amesema Fatma.
Fatma amesema “mahakama na Jaji Mkuu wana haki ya kuanzisha mahakama inayochunguxa vifo vya wanaokufa katika mazingira tatanishi. Watu wanakufa jela hakuna mahakama ya kuchunguza.”
Wakati huo huo, Fatma ameitaka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP), kushughulikia kesi zilizokaa muda mrefu kwa sababu ya uchunguzi wake kutokamilika ili kutoa haki kwa watuhumiwa.
Ametoa wito huo baada ya Sheikh Said Ulatule, kufariki dunia kwa matatizo ya moyo, akiwa mahabusu alikokuwa anashikiliwa kwa tuhuma za ugaidi tangu 2016.
Katika hatua nyingine, Karume ameshauri Jeshi la Polisi kufuata sheria katika shughuli za ukamataji watuhumiwa mbalimbali ikiwemo kuwapa dhamana kwa wanaostahili na kuwapa haki ya kuwasiliana na ndugu zao.
Ameshauri Jeshi la Polisi kutoa taarifa kwa wakati pindi linapokamata watuhumiwa ili kuondoa wasiwasi kwamba wametekwa na wasiojulikana.
Leave a comment