BENKI ya Exim Tanzania imeadhimisha miaka 25 tangu kuanzishwa kwa hafla fupi iliyolenga kutambua jitihada na mchango wa wafanyakazi wa benki hiyo katika kufanikisha ustawi wa benki hiyo. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Maadhimisho hayo yaliyofanyika leo tarehe 16 Agosti, 2022 Makao Makuu ya benki hiyo jijini Dar es Salaam na kuhudhiriwa na viongozi waandamizi na wafanyakazi wa benki hiyo.
Aidha, utambuzi na pongezi za heshima zilitolewa kwa watumishi waliohudumu katika benki hiyo tangu kuanzishwa kwake miaka 25 iliyopita.
“Benki ya Exim imejitolea kwa dhamira yetu ya dhati kuwaweka wadau wetu muhimu wakiwemo wafanyakazi na wateja mbele,” alisema Jaffari Matundu, Ofisa Mtendaji Mkuu wa benki hiyo.
“Wafanyikazi wetu ndio wanaosimamia dira yetu ya kila siku wakitoa huduma ya kipekee kwa wateja wetu. Tukio hili linatoa fursa kwetu kutambua juhudi zao za pamoja, na kusherehekea mafanikio ambayo yasingewezekana bila wao.’’
Alisema maadhimisho hayo yanahusisa matawi yote ya benki hiyo nchi nzima na itahusisha mpango wa benki hiyo katika kusaidia jamii kwa namna mbalimbali.
Kwa mujibu wa Matundu benki hiyo imejipanga zaidi kuendelea kuwapa wateja wake bidhaa na huduma za kibunifu huku ikijiweka katika nafasi ya ushindani mkubwa katika ukanda wa Afrika Mashariki.
“Ili kuendelea kufikia malengo yetu, miaka ijayo tunahitaji kuwa na uvumbuzi zaidi, teknolojia salama na yenye ufanisi, huduma bora kwa wateja na zaidi ya yote, ushirikiano mkubwa na msaada wa wateja wetu, washirika wa biashara, mamlaka mbalimbali na wadau wengine wote,” alitaja.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mkuu wa Kitengo cha Rasilimali Watu wa Benki ya Exim, Fredrick Kanga, aliwashukuru wafanyakazi hao kwa mchango wao katika ukuaji wa benki hiyo huku akibainisha kuwa uongozi unaheshimu na kutambua umuhimu wa kila mfanyakazi katika kuleta maendeleo ya benki hiyo.
Alisema muda mrefu wa utumishi miongoni mwa baadhi ya wafanyakazi wa benki hiyo unaonyesha kiwango cha uaminifu na kujitolea kwa pande zote mbili yaani wafanyakazi wenyewe pamoja na uongozi wa Benki na hivyo kudhihirisha uaminifu baina ya pande hizo muhimu.
“Tangu mwanzo, tumefungua milango yetu kwa vijana ambao wanataka kuishi ndoto zao na kufuata kazi zinazoakisi ujuzi na shauku yao,’’ alisema.
Alibainisha kuwa benki hiyo ilianzishwa mwaka 1997 jijini Dar es Salaam ikiwa ni huduma rafiki zenye ubunifu ikiwa na wafanyakazi 16 tu wanaojituma sambamba na wateja waaminifu kwa huduma za benki hiyo.
“Leo hii, Benki ya Exim imekua na kuwa moja ya benki imara zaidi nchini ikiwa na matawi 30 maeneo mbalimbali nchini Tanzania na zaidi ya wafanyakazi 900 katika mataifa matano ambao bado wanaendeleza utamaduni uliotukuka wa kusaidia familia na biashara kuimarika kiuchumi,’’ aliongeza.
Akiwashuhudia mbele ya wafanyakazi wengine wa benki hiyo, Eugine Massawe, Mkuu Uendeshaji wa matawi ya benki hiyo ambaye ni mmoja wa watumishi wa benki hiyo waliohudumu kwa kipindi cha miaka 25 alisema uhusiano wake na benki hiyo katika kipindi chote ni wa ushirika zaidi.
“Na ninafuraha kuendelea kujitoa niwezavyo kwa ushirikiano huu kwa manufaa ya benki, na pia kwa ajili yangu mwenyewe. Malengo yangu ya kibinafsi na kitaaluma yanawiana na ramani ya ukuaji wa muda mrefu ya benki ya Exim na mazingira mazuri ya kazi yananipa motisha zaidi” alisema.
Leave a comment