JUMUIYA ya kiuchumi ya nchi za Afrika magharibi ECOWAS imesimamisha uanachama wa Guinea baada ya wanajeshi wa nchi hiyo kuiangusha serikali ya Rais Alpha Conde. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Jumuiya ya ECOWAS imeitaka Guinea irejee kwenye utaratibu wa kawaida wa katiba.
Kutokana na hatua hiyo Guinea kwa sasa imesimamishwa kwenye mabaraza yote ya kupitisha maamuzi ya jumuiya hiyo.
Jumuiya ya kiuchumi ya nchi za Afrika magharibi pia imetoa mwito kwa Guinea wa kuanzisha mchakato wa kurejea haraka kwenye uongozi wa kikatiba.
Waziri wa mambo ya nje wa Burkina Faso, Alpha Barry amesema baada ya mkutano wa viongozi wa nchi 15 za ECOWAS kwamba jumuiya hiyo inataka kuachiwa huru mara moja kwa rais Alpha Conde aliyekamatwa na wanajeshi waliotwaa madaraka.
Ujumbe wa upatanishi wa jumuiya ya ECOWAS unatarajiwa kuwasili leo tarehe 9 Septemba katika mji mkuu wa Guinea, Conakry.
Umoja wa Mataifa pamoja na Umoja wa Afrika pia zimelaani mapinduzi ya kijeshi nchini Guinea.
Leave a comment