RAIS John Magufuli ameicharukia kampuni ya ukandarasi ya Dott Service, kwa kuchelewa kumaliza utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa barabara ya Mtwara – Mnivata. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Akizungumza katika uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa barabara ya Mtwara – Mvinata yenye urefu wa kilomita 50 leo tarehe 3 Aprili 2019 mkoani Mtwara, Rais Magufuli ameagiza mkandarasi huyo kufanya kazi usiku na mchana ili kukamilisha ujenzi huo.
Rais Magufuli ameagiza Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kutompa kazi ya ukandarasi kampuni ya Dott Service kutokana na historia ya kusuasua katika kutekeleza miradi ya ujenzi wa barabara ya serikali.
“Sijafurahishwa na kasi ya utekelezaji wa mradi, huu mradi haujaenda vizuri.Mkandarasi wa hapa tangu mwaka jana anahangaika na km 50 angepewa 200 angechukua muda gani, rekodi ya mkandarasi huyu si nzuri, kuna mradi alichelewesha halafu mnampa tena?” amehoji Rais Magufuli na kuongeza;
“Huwezi kusubiri miaka mitatu barabara ya kilomita 50. Kila siku yuko ‘site’ haiwezekani, mkandarasi aanze kufanyakazi usiku na mchana.
“Mkandarasi ameingia kwenye 18 zangu, msimpe kazi nyingine Mkandarasi huyu mpaka akimaliza kazi hii hata kama akishinda zabuni.”
Aidha, Rais Magufuli amewataka wakandarasi nchini kukamilisha miradi wanayokabidhiwa kwa wakati husika, na kuagiza wizara ya ujenzi kuwachukulia hatua wakandarasi wanaokiuka mikataba yao kwa kuchelewa kukamilisha ujenzi wa miradi hiyo.
Katika hatua nyingine, Rais Magufuli aliagiza Wizara ya Ujenzi kuhakikisha katika bajeti ya mwaka huu wa fedha wanatenga fedha kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami, kwa urefu wa kilomita 50 .
Leave a comment