BALOZI wa Tanzania nchini Sweden, Dk. Willibroad Slaa, amerejea jijini Dar es Salaam na kufanya mazungumzo na Rais John Pombe Magufuli. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Haikuweza kufahamika mara moja, kilichojadiliwa katika mazungumzo kati ya Dk. Slaa na Rais Magufuli.
Hata hivyo, katika siku za karibuni iliripotiwa kwenye vyombo vya habari vya Magharibi na mitandao ya kijamii, kuwa balozi huyo anayehudumu kwenye nchi za Sweden na Finland ameitwa Ikulu ya Sweden “kufokewa” kufuatia hatua ya nchi yake kutoheshimu haki za binadamu.
Dk. Slaa ambaye alikuwa katibu mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), hadi Agosti mwaka 2015, aliteuliwa kuwa balozi na Rais Magufuli katikati ya mwaka huu.
Rais Magufuli alimteuwa Dk. Slaa kuwa balozi, kipindi ambacho alikuwa akiishi “uhamishoni” nchini Canada.
Dk. Slaa alipelekwa “uhamishoni” nchini Canada na aliyekuwa mchumba wake, Josephine Mushumbuzi.
Kwa sasa, taarifa zinasema, wapenzi hao wawili – Dk. Slaa na Josephine – tayari wamefunga ndoa kwenye kanisa moja nje ya nchi.
Josephine alichukua uamuzi wa kumpeleka uhamishoni Dk. Slaa, kufuatia kushindwa kwa mpango wake wa kumng’ang’aniza kuwa mgombea urais wa Chadema/ Ukawa kwenye uchaguzi mkuu wa 25 Oktoba 2015.
Dk. Slaa ambaye ni amewahi kuwa Padri wa Kanisa Katoliki na kuhudumu kwenye nafasi ya Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu la Tanzania (TEC), alikuwa mmoja wa wanasiasa wenye ushawishi mkubwa nchini.
Mbali na kuwahi kugombea urais katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010, amepata kuwa mbunge wa Karatu kwa vipindi vitatu mfululizo.
Leave a comment