MSIMAMIZI wa uchaguzi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk Ali Mohamed Shein ambaye ni Rais mstaafu wa Zanzibar leo tarehe 7 Disemba, 2022 amemtangaza, Dk. Samia Suluhu Hassan kuwa Mwenyekiti wa Chama hicho kwa mara nyingine baada ya kupigiwa kura za ndio 1914 kati 1915. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Samia ambaye alirithi nafasi hiyo kutoka Rais wa awamu ya tano Dk. John Magufuli aliyepoteza maisha Machi, 2021, amechaguliwa kwa mara ya kwanza kwa kupigiwa kura na kuwa mwanamke wa kwanza kuongoza chama hicho tangu kiasisiwe mwaka 1977.
Abdulrahman Kinana naye amechaguliwa kuwa Makamu mwenyekiti wa CCM Bara na kutetea nafasi hiyo baada ya kupigiwa kura za ndio 1,913 kati ya 1915 huku Rais wa Zanzibar, Dk Hussein Mwinyi akichaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti wa Zanzibar,baada ya kupigiwa kura za ndio 1,912.
Aidha, katika uchaguzi huo pia idadi kubwa ya nafasi za wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) zimechukuliwa na mawaziri .
Baadhi ya mawaziri hao walioshinda ni pamoja na Angelah Kairuki ambaye ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Tamisemi), Dk. Ashatu Kijaji (Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwezekezaji), Angelina Mabula (Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi).
Mkutano wa 10 wa CCM umefanyika leo tarehe 7 Disemba, 2022 jijini Dodoma.
Leave a comment