WAZIRI wa Fedha na Mipango, Dk. Mwigulu Nchemba amesema katika kipindi cha mwaka mmoja wa Rais Samia Suluhu Hassan madarakani amefanya mambo mengi ambayo yameleta mabadiliko yanayoonekana hadi mitaani kwa watu kuwa na fedha mifukoni. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha … (endelea).
Ameyasema hayo leo Jumanne tarehe 15 2022 jijini Arusha, akielezea mafanikio ya Wizara ya Fedha na Mipango katika kipindi cha mwaka mmoja wa Serikali ya awamu ya sita.
Dk. Nchemba amesema licha ya uchumi kushuka kutoka wastani wa asilimia 7 mwaka 2019 hadi asilimia asilimia 4.8 mwaka 2020, kutokana na athahari za janga la Virusi vya Uviko -19, lakini Rais Samia ameanza kuchukua hatua na kuwezesha kuongezeka hadi asilimia 4.9 mwaka 2021.
Amesema kutokana na hatua zinazoendelea kuchukuliwa matarajio ni kufikia wastani wa asilimia 5 mwaka 2022 na kwamba Benki ya Dunia imetabiri kufikia hadi asilimia 5.5.
Amesema haya yote yamewezekana kwa uwekezaji uliofanywa kwenye ujenzi wa miundombinu ya barabara, reli, bandari, na kuweka mazingira mazuri kwa waekezaji nchini.
Ametaja maeneo yaliyoonesha tofauti kuwa ni ongezeko la mikopo kwa sekta binafsi kutoka asilimia 3.3 Desemba 2020 hadi asilimia 10 Desemba 2021, “ maana yake kuna shughuli zimefanyika kwenye sekta binafsi na ajira zimeongezeka huko na kama ajira zimeongezeka mapato ya wananchi yameongezeka.”
Ameongeza kuwa badiliko mengine ni kwenye mikopo chechefu kupungua kutoka asilimia 9.3 mwaka 2020 hadi asilimia 8.2 2021, “ hii maana yake watu waliokuwa wanashindwa kurejesha mikopo wamepungua na hii ni baada ya agizo la Rais la kulipa madeni yanayodaiwa ikiwemo kulipa wazabuni, wakandarasi na madeni mengine ya sekta binafsi na taasisi zinazotoa huduma kwa serikali.”
Amefafanua kuwa matumizi ya serikali yanavutia matumizi ya mtu mmoja mmoja ambao nayo inaongeza uwekezaji na uwekezaji unaongeza ajira na hivyo fedha kuwafikia wananchi moja kwa moja.
Mabadiliko mengine ni kuongeza kwa ukwasi kwa wastani wa asilimia 9.5, “ hii ina maana zile Sh 1.3 trilioni ilikwenda vijijini na wakandarasi wanatokea kule kwenye vijiji na hivyo tuna uhakika fedha zimefika mifukoni mwa watu kule walipo.”
Amesema akiba ya fedha za kigeni imeongezeka kwa kiwango cha kuweza kuagiza bidhaa kwa miezi 6.6 huku mapato yakiongezeka hadi Sh 15.9 trilioni kufikia Februari 2022 sawa na asilimia 93.5 ya lengo kutoka Sh 13 trilioni huku makusanyo ya mwezi Desemba 2021 yakifikia Sh 2.5 trilioni “kiwango ambacho hakijawahi kufikiwa katika historia ya Mamlaka ya Mapato.”
Grazie ndugu nchemba kwa kutimzmiza wajibu wa kikazi sasa kwetu ni furaha