MAKAMU wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Othman Masoud Othman, amesema kwamba ushirikiano baina ya Wataalamu na watafiti mbalimbali, unahitajika hasa katika nyanja ya mafunzo na Teknolojia, maabara na vifaa pamoja na machapisho ili kuendeleza vyema kazi hiyo. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Othman ameyasema hayo leo tarehe 9 Agosti, 2022 katika mkoa wa Mjini Magharibi Unguja wakati akisoma kwa niaba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi wakati akifungua Kongamano la 16 la kimataifa la Jumuiya ya Wanazuoni na Watafiti wa Mambo ya Kale.
Amesema taaluma ya Mambo ya Kale na Urithi wa Utamaduni unagusa sekta zote za kiuchumi, Kijamii, kisiasa, Teknolojia, Mazingira yakiwemo magonjwa mbalimbali, na kwamba ni tegemeo kubwa la taifa kuweza kufahamu nchi ilikotoka, ilipo sasa na inakokwenda kwani tafiti zinatoa mchango mkubwa katika utekelezaji wa malengo yanayopangwa nchini.
Aidha, Othman amewashauri watafiti kuwa msaada mkubwa kwa kutafsiri matokeo ya tafiti zao kwa kuyachapisha, sambamba na mapendekezo yao ya kuboresha maeneo ya tafiti hizo kwa lugha nyepesi ili kwa pamoja iwe ni sehemu ya vivutio vya utalii.
Makamu huyo amefahamisha kwamba hatua hiyo itasaidia kuimarisha matumaini ya Zanzibar, Tanzania na kwingineko Afrika, kupokea wataalii wengi zaidi kama zilivyo nchi nyengine nyingi duniani na kuchangia kuongeza mapato ya taifa na hivyo kukuza uchumi kwa haraka.
Othman amewakaribisha watafiti mbalimbali duniani, kufanya tafiti zao Zanzibar hasa katika masuala ya Akiolojia ya baharini kwa kuzingatia kuwa Serikali ya awamu ya nane, moja ya sera yake muhimu ni uchumi wa Buluu na kwamba utajiri wa urithi uliopo baharini unaweza kutumika kama fursa muhimu ya kukuza sekta hiyo hapa Zanzibar.
Othman amefahamisha kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inatoa kipaumbele katika masuala ya Utafiti wa namna hiyo, na ndio maana imeunda Wizara kamili inayoshughulikia mambo ya Kale, na kwamba ni fursa kwa wataalamu kufanya tafiti mbali mbali za aina hiyo hapa Zanzibar.
Aidha, amewataka washiriki wa kongamano hilo kutoka nchi mbali mbali duniani, kutenga muda wao kutembelea vivutio mbali mbali vya utalii vilivyopo Zanzibar na Tanzania kwa jumla na itasaidia kuona hali ya ukarimu na usalama mzuri uliopo nchini Tanzania.
Pia amewaeleza kwamba kufanyika kwa kongamano hilo hapa Zanzibar iwe ni fursa muhimu kwa watafiti kubaini maeneo tofauti ya kufanyiwa utafiti, ili kwa kushirikiana na Wizara na Vyuo Vikuu waweze kufanya tafiti tofauti ambazo zinahitajika kwa mchango wa maendeleo.
Mapema Waziri wa Utalii na Mambo ya Kale Zanzibar Mhe. Simai Mohammed Said, amesema kwamba Serikali kupitia wizara yake ipo tayari kutoa mashirikiano yatakayohitajika, katika kufanikisha kufanyika tafiti mbali mbali zinazohusu mambo ya Kale Zanzibar.
Kongamano hilo limehudhuriwa na washiriki mbali mbali kutoka nje ya Tanzania, wakiwemo Kenya, Uganda, Zimbabwe, Aljeria, Ethiopia, Botswana, Afrika Kusini na Zambia.
Nyingine ni DRC Congo, Senegal, Nageria, Mali, Moroco na Wenyeji Tanzania ikiwemo Zanzibar chini ya maandalizi ya mashirikiano baina ya Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar – (SUZA), Chuo Kikuu cha Dar es Salaam – (UDSM), Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) pamoja na Wizara inayoshughulikia Utalii na Mambo ya Kale Zanzibar.
Leave a comment