RAIS wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar (SUK), Dk. Hussein Mwinyi amesema, hatojali mtoto wa mtu katika maamuzi magumu atakayochukua ingawa hatofukua makaburi. Anaandika Mwandishi Wetu, Zanzibar…(endelea).
Akizungumza katika Ukumbi wa Fiedel Castro, Chakechake visiwani humo leo tarehe 17 Desemba 2020, wakati wa kutoa shukrani zake kwa wanachama na taasisi za Chama Cha Mapinduzi (CCM), amesema Wazanzibari wasitaharuki kwa maamuzi atakayochukua.
“Katika kuhakikisha ahadi zetu tulizotoa zinakamilika, nataka niseme katika kipindi hiki cha kwanza lazima tutafanya maamuzi magumu. Naomba mtulie, msitaharuki, nataka kukuhakikishieni maamuzi nitakayofanya yana lengo moja tu, kuthibiti.
“Sitafuti mchawi wala sifukui makaburi lakini yako mambo tusipoyafanya kwa maamuzi magumu, huko tunakokwenda nako ni kugumu,” amesema Dk. Mwinyi huku akiwataka wakazi wa visiwa hivyo viwili (Unguja na Pemba) kumvumilia.
Amesema, serikali yake haina uvumilivu na watu wala rushwa, wahujumu uchumi pia wanaokula mali ya umma kwa kuwa, asipofanya sasa, mbele ya safari itakuwa tabu.
Rais huyo amesema, Zanzibar kila mtu unayeweza kumgusa, unaweza kuambiwa ‘ni mtoto wa fulani’ na kwamba hilo kwake hatolizingatia.
Na kwamba, muda aliokaa madarakani tayari kila eneo alilogusa, linanuka rushwa na kwamba, nchi inaendelea kufilisiwa kwa vitendo vya ufisadi.
Mwenyekiti huyo wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar amesema, ili kutimiza ahadi zake alizotoa katika kampeni za Uchaguzi Mkuu uliofanyika tarehe 28 Oktoba 2020, lazima achukue uamuzi mgumu hasa baada ya kushuhudia uozo.
Dk. Mwinyi amesema, lengo la uamuzi huo ni kuhakikisha anadhibiti matumizi mabaya ya fedha za miradi ya maendeleo.
“Leo tunazungumzia miradi ya maendeleo ya fedha nyingi, tunazungumzia miradi ya maendeleo ya fedha nyingi, zaidi ya Dola za Marekani Mil. 93 zinakwenda katika mradi wa maji unaonedelea.
“Na kuna miradi itakayokuja inayogharimu Dola 110 Mil. tusipochukua maamuzi magumu sasa, hizi fedha zitafujwa,” amesema na kuongeza:
“Iko miradi ya maji, umeme na barabara. Nataka niahidini tutaisimami ili tuweze kupata thamani katika fedha tutakazotoa.”
Leave a comment