MAKAMU mpya wa Rais wa Tanzania, Dk. Phillip Mpango, amemuahidi Rais wa nchi hiyo, Samia Suluhu Hassan, kuwa katika utekelezaji wa majukumu yake mapya, hatakuwa msaliti kama Yuda Eskarioti alivyomsaliti Yesu Kristo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Mwanasiasa huyo ametoa ahadi hiyo leo Jumatano tarehe 31 Machi 2021, baada ya kuapishwa kuwa Makamu wa Rais, Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma.
Dk. Mpango ameapishwa kumrithi Mama Samia, baada ya mwanamama huyo kuapishwa kuwa Rais wa Tanzania, kufuatia kifo cha Hayati Dk. John Magufuli, kilichotokea tarehe 17 Machi 2021, kwenye Hospitali ya Mzena, Makumbusho mkoani Dar es Salaam.
“Wiki hi Wakristo tunasherehekea Jumaa Kuu na siku ya kesho mtu anaitwa Yuda Eskarioti kwenye Biblia alipomsaliti Yesu kwa vipande 30 vya fedha. Rais nataka nikuhakikishie sitakuwa kama huyo Yuda,” amesema Dk. Mpango.
Dk. Mpango ameahidi “nikuahidi nitakuwa msaidizi muaminifu na muadilifu lakini mzalendo wa kweli kwa nchi yangu.”
Akitoa ahadi zake kwa Rais Samia, Dk. Mpango amesema, atatekeleza kwa bidii majukumu yake ya Makamu wa Rais wa Tanzania, huku akimualika Rais Samia amtume wakati wowote kwani yuko tayari kuchapa kazi.
“Nitatekeleza kwa bidii na weledi kazi zote utakazoniagiza pamoja na majukumu mengine kama yalivyoelekezwa kwenye Katiba Ibara ya 47, nitatekeleza majukumu haya chini ya uongozi wako,” amesema Dk. Mpango
“Niko tayari kuchapa kazi, nitume mchana na usiku hususan kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya 2020, uliyoinadi nchi nzima katika kampeni.”

Kabla ya kuteuliwa kuwa Makamu wa Rais, Dk. Mpango alikuwa Waziri wa Fedha na Mipango, ambayo kwa sasa Dk. Mwigulu Nchemba ameteuliwa kuiongoza.
Mabadiliko hayo yamekuja siku kadhaa tangu Rais Samia aapishwe Ikulu ya Dar es Salaam, tarehe 19 Machi 2021.
Rais Samia alikuwa makamu wa rais kwa miaka mitano na miezi mitano mfululizo (Novemba 2015 hadi Machi 2021).
Mwili wa aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano wa Tanzania, Dk. Magufuli ulizikwa nyumbani kwao Chato mkoani Geita.
Leave a comment