MAKAMU wa Rais wa Tanzania, Dk. Phillip Mpango, amewataka wananchi wa Mkoa wa Mtwara, kuwa makini dhidi ya wanamgambo wa kundi la kiislamu, wanaofanya vitendo vya ugaidi nchini Msumbiji. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mtwara … (endelea).
Dk. Mpango ametoa wito huo leo Jumatatu, tarehe 26 Julai 2021, akiweka jiwe la msingi katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Kusini, mkoani Mtwara.
Makamu huyo wa rais, amewaomba wananchi wawe macho dhidi ya wanamgambo hao, huku akiwataka watoe taarifa katika vyombo vya ulinzi na usalama, wanapoona wageni katika mkoa huo.
“Mtwara tuko mpakani na mnafahamu hali kwa majirani zetu pale Msumbiji ilivyo, nataka kuwaomba kila mahali ambako tumewekeza kama Taifa tuwe macho kuchunga. Mkianza kuona sura hamzielewi mtoe taarifa kwa vyombo vya ulinzi na usalama,” amesema Dk. Mpango.
Wanamgambo hao wa kiislamu wanaoshukiwa kuwa na uhusiano na Kundi la Al Shabab, wamevamia Mji wa Cabo Delgado, ulioko mpakani mwa Tanzania na Msumbiji.
Tangu wanamgambo hao wavamie eneo hilo, wanadaiwa kuuwa maelfu ya watu, huku zaidi ya laki nane, wakikimbia makazi yao.
Hivi karibuni Wanajeshi wa Rwanda, walifanikiwa kuwauwa wanamgambo zaidi ya 30, kufuatia doria walizofanya katika msitu ulio karibu na mji wa Bandari ya Palma.
Leave a comment