Friday , 19 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Dk. Mpango ahofia vita ya kiuchumi ‘umasikini bado mkubwa’
Habari za Siasa

Dk. Mpango ahofia vita ya kiuchumi ‘umasikini bado mkubwa’

Dk. Phillip Mpango, Waziri wa Fedha na MIpango Tanzania
Spread the love

DAKTARI Phillip Mpango, Waziri wa Fedha na Mipango wa Tanzania ameahidi kutumia vyema rasilimali zilizopo nchini kupunguza umasikini, badala ya kutegemea fedha za wafadhili wa maendeleo. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).

Dk. Mpango ameyasema hayo leo Jumatatu tarehe 16 Novemba 2020 baada ya kuapishwa na Rais John Magufuli kuwa Waziri wa Fedha na Mipango, Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma.

Waziri huyo wa fedha na mipango ametoa kauli hiyo wakati anazungumzia vipaumbele vyake katika utekelezaji wa majukumu yake kwenye wizara hiyo, ambayo alihudumu katika Baraza la mawaziri lililopita kabla ya kuvunjwa.

Dk. Mpango amemuahidi Rais Magufuli atahakikisha mapato ya Serikali yanaongezeka kwa kutumia vyema fursa zilizopo kusukuma maendeleo ya Watanzania.

https://youtu.be/rX8CJRibAmo

Amesema, Tanzania haitashinda vita ya kiuchumi kama kila mmoja hatatimiza wajibu wake.

“Vita vya kiuchumi ni halisi na mimi nakuahidi nitakuwa askari wako kwenye vita hii ya kiuchumi, na muhimu mapato ya Taifa lazima yaongezeke, kuombaomba umetufundisha tuache na mimi nimechoka kuomba, fursa ziko tele za kusuma maendele ya Watanzania,” amesema Dk. Mpango ambaye pia ni Mbunge wa Buhigwe mkoani Kigoma,

Aidha, Dk. Mpango amewaomba Watanzania watimize wajibu wao wa kulipa kodi ili Serikali ipate fedha za kutosha kujiendesha na kuachana na fedha za wafadhili.

“Kwa ajili ya vita ya kiuchumi, kila mmoja ahakikishe analipa kodi ipasavyo,” amesema Dk. Mpango.

Dk. Mpango amewaagiza watumishi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuwa waaminifu katika utendaji kazi wao na kuachana na njia za udanganyifu au kuwatoza kodi kubwa wafanyabishara kinyume na sheria.

Dk. Philip Mpango

“Nawaomba watendaji wa TRA, maandiko yanasema tutoze kodi kama ilivyoamliwa, tusitoze kodi kwa ziada au kuweka mfukoni, hatutashinda vita hii ya kiuchumi, inawezekana kila mtu akitimzia wajibu wake, kujitegemea wenyewe,” amesema Dk. Mpango.

Akielezea viapumbele vyake katika utekelezaji wa majukumu yake, Dk. Mpango amesema, atasimamia vyema ukusanyaji wa mapato sambamba na matumizi yake, ili kudhibiti mianya ya upotevu wa fedha za umma kupitia utekelezwaji wa miradi ya maendeleo.

“Nitasimamia hili tukusunye mapato ya Serikali kwa ubunifu zaidi, matumizi ya Serikali ni eneo ambalo yako matumzi yasiyo na tija, nitalisimamia hili,” amesema Dk. Mpango.

Waziri Mpango amesema, kupitia Kampeni za Uchaguzi Mkuu uliofanyika tarehe 28 Oktoba 2020, alibaini kwamba nchi inapoteza fedha nyingi kupitia miradi ya maendeleo.

Amewaonya watendaji watakaoendelea kuiba fedha za umma kwa kufanya udanganyifu katika gharama za ujenzi wa miradi hiyo.

“Nilipoenda katika kampeni bado kuna shida katika miradi ya maendeleo, bado tunaibiwa. Nitasimamia nchi nzima tuokoe fedha za wanyonge zifanye kazi yake, kwa kuwa umenipa kisu watupishe tutende kazi nchi yetu isonge mbele,” amesema Dk. Mpango.

Dk. Mpango amesema ataongoza Wizara ya Fedha na Mipango na taasisi zilizo chini yake kufanya majadiliano na sekta binafsi ili kuondoa changamoto inazozikabili, ipate nafasi ya kushiriki kwenye ujenzi wa uchumi wa nchi.

“Ulisisitiza kurudisha majadiliano kati ya wizara zote na Serikali nzima pamoja na sekta binafsi. Kama uchumi wa kweli ni sekta binafsi, hii nitajipanga upya ili sekta binafsi ipate nafasi yake katika ujenzi wa nchi yetu,”amesema Dk. Mpango.

Wakati huo huo, Dk. Mpango ameahidi kusimamia wizara yake vyema ili kupunguza umasikini wa wananchi hasa walioko sehemu za vijijini.

“Pamoja na kuwa tumefanikiwa kuifikisha Tanzania yetu kuwa nchi yenye hadhi ya kipato cha kati bado huko tulipoenda kwenye kampeni umasikini bado mkubwa. Bado tunahitaji kufanya kazi kwa bidii kuwatumikia watu wetu,” amesema Dk. Mpango.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

Wabunge waikalia kooni TAKUKURU Bungeni

Spread the love  BAADHI ya wabunge wamelia na changamoto za utendaji wa...

Habari za SiasaTangulizi

Mpina ataka Waziri Majaliwa ajiuzulu, akosoa teuzi za mawaziri

Spread the love  MBUNGE wa Kisesa, Luhaga Mpina, amemtaka Waziri Mkuu, Kassim...

Habari za Siasa

CCM yakemea ufisadi, yaipa kibarua TAKUKURU

Spread the love  CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimekemea vitendo vya ubadhirifu wa...

Habari za Siasa

Bajeti ya Ikulu 2024/25 kuongezeka, bunge laombwa kurudhia Sh. 1.1 trilioni

Spread the love  WIZARA ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa...

error: Content is protected !!