Wednesday , 24 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Dk. Mashinji: Lowassa anajua anachokifanya, Prof. Lipumba acheeeka
Habari za Siasa

Dk. Mashinji: Lowassa anajua anachokifanya, Prof. Lipumba acheeeka

Spread the love

HATUA ya Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Ngoyai Lowassa kutangaza kurejea katika Chama Cha Mapinduzi (CCM) jana tarehe  Mosi Machi 2019, kumeibua mjadala mpana uliobeba hisia tofauti. Anaripoti Bupe Mwakiteleko … (endelea).

Akizungumza na MwanaHALISI ONLINE leo tarehe 2 Machi 2019 Dk. Vincent Mashinji amesema, sio jmabo la ajabu kwa Lowassa kurejea CCM na kwamba, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kitaendelea kuwa imara.

Dk. Mashinji amesema, Lowassa bila shaka ni mtu mzima na anajua nini anachokifanya, ndio maana amefikia uamuzi wa kurudi kule alikotoka.

“Lowassa ni mtu mzima, anajua anachokifanya. Kuondoka kwake hakuwezi kuteteresha Chadema, namtakia kheri huko aendako,” amesema Dk. Mashinji.

Wakati Dk. Mashinji akieleza hayo, Prof. Ibrahim Lipumba, Mwenyekiti wa CUF-Taifa anayetambuliwa na Msajili wa Vyama vya Siasa amenukuliwa na chombo kimoja cha habari akisema ‘nilijua.’

Prof. Lipumba alikumbusha hoja zake wakati akijiuzulu uenyekiti wa CUF kwamba, uamuzi wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) kumpitisha Lowassa kuwa mgombea wao, waliteua mgombea urais wa pili kutoka CCM baada ya Dk. John Magufuli.

“Nilisema toka awali, kwenye uchaguzi wa 2015 kulikuwa na wagombea wawili wa CCM. Si Magufuli peke yake, Lowassa alikuwa mgombea wa CCM pia,” alisema.

Pia ameeleza kushangazwa na hatua ya Lowassa kurudi CCM wakati aliyemkaribisha Chadema (Freeman Mbowe) akiwa mahabusu.

Lowassa aliondoka CCM na kujiunga na Chadema, kupitia mkutano wake na waandishi wa habari wa tarehe 28 Julai 2015, katika hoteli ya Bahari Beach jijini Dar es Salaam.

Alichukua hatua hiyo, wiki moja baada ya jina lake kuenguliwa katika orodha ya wagombea urais wa CCM.

Aliwaambia waandishi wa habari kuwa  CCM haikumtendea haki katika kupitisha majina ya wagombea urais, hivyo hawezi kuendelea kubaki kwenye chama hicho.

“Niliwekewa mizengwe, kuhakikisha jina langu halifiki Kamati Kuu na Halmashauri Kuu (NEC). Nia yangu ni kuleta mabadiliko na kuondoka kwangu na kujiunga na Chadema, ni kuendeleza dhamira hiyo,” alieleza.

Aliongeza, “CCM siyo Baba yangu, wala siyo Mama yangu. Kama Watanzania wameyakosa mabadiliko CCM, basi watayatafuta kwingine. Ninaondoka. Sijakurupuka.”

Katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, Lowassa aligombea urais kupitia UKAWA na kutangazwa kushika nafasi ya pili nyuma ya Dk. Magufuli. Hata hivyo, mwenyewe amekuwa akidai mara kadhaa kuwa kura zake ziliibwa.

Vyama vilivyomuunga mkono Lowassa katika kinyang’anyiro hicho, ni Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), NCCR- Mageuzi, Chama cha Wananchi (CUF) na National Legue Democrat (NLD).

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za SiasaTangulizi

Biteko ataja vipaumbele 7 bajeti nishati 2024/25

Spread the love  NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Doto...

Habari MchanganyikoHabari za Siasa

Mwekezaji amwaga bil. 39 kujenga viwanda 3 vya uchenjuaji

Spread the loveKampuni ya Mineral Access System Limited (MAST) inayoiwakilishwa kampuni ya...

Habari za SiasaTangulizi

Mpwa wa Magufuli mbaroni kwa kusambaza picha za utupu

Spread the loveJESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limewakamata...

Habari za Siasa

Serikali kuanzisha mradi wa Gridi ya maji ya Taifa

Spread the loveWaziri wa Maji, Jumaa Aweso amesema katika mwaka wa fedha...

error: Content is protected !!