MBUNGE wa Vunjo kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Charles Kimei, amefikisha bungeni kilio cha waongoza watalii katika Mlima Kilimanjaro, kuhusu kutolipwa stahiki zao. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma…(endelea).
Dk. Kimei amefikisha kilio hicho leo Jumatano tarehe 3 Februari 2021, bungeni jijini Dodoma.
Dk. Kimei ameihoji Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kunakuwepo mwongozo unaoelekeza mawakala wa utalii katika mlima huo (Tour Operator), kuwalipa ujira stahiki wapagazi, wapishi na waongoa misafara, wanaowaajiri.
“Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kunakuwepo na mwongozo unaotekelezwa kwa Tour Operators wanaopandisha watalii Mlima Kilimanjaro wanaoajiri wapagazi, wapishi na waongoza misafara kwa kuwalipa ujira stahiki,” amehoji Dk. Kimei.
Akijibu swali hilo, Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Damas Ndumbaro, amesema Serikali imeshatoa mwongozo kwa mawakala hao tangu mwaka 2015, ambao unawaelekeza mawakala hao kuwalipa ujira stahiki waajiriwa wao.
Amesema katika muongozo huo, Serikali iliagiza muongoza watalii alipwe Dola za Marekani 20 kwa siku (Sh. 40,000), mpishi akilipwa Dola 15 (Sh.30,000) na mpagazi Dola 10 (Sh.20,000), kwa siku.
Hata hivyo, Dk. Kimei amesema utekelezwaji wa muongozo huo una changamoto, kwa kuwa baadhi ya mawakala wa utalii hawawalipi waajiriwa wao viwango hivyo.
Kutokana na changamoto hiyo, Dk. Kimei amesema Serikali imeweka mikakati mbalimbali kuhakikisha viwango vya malipo vinavyoelekezwa na muongozo huo vinalipwa kwa wahusika.
“Baadhi ya mikakati hiyo ni pamoja na kushirikiana na Wizara ya Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu (Idara ya kazi), kuandaa mikataba ya kisheria ambapo mawakala wa utalii husaini pamoja na waongoza watalii, wapagazi na wapishi wanaoajiriwa kabla ya kuanza kazi,” amesema Dk. Ndumbaro.
Dk. Ndumbaro amesema, mikataba hiyo inaainisha viwango vya malipom, idadi ya siku na jumla ya malipo wanayostahili watu hao kulipwa baada ya kufanya kazi.
“Nakala moja ya mkataba huu, hukabidhiwa kwenye lango la kupandia mlima, nakala nyingine hupewa waajiriwa (waongoza watalii, wapishi na wapagazi) na nakala moja hubaki kwa wakala wa utalii; (ii) Idara ya Kazi imekuwa ikihimiza waajiriwa kutokuanza kazi bila ya kuwa na mikataba,” amesema Dk. Ndumbaro.
Sambamba na hilo, Dk. Ndumbaro amesema Idara ya Kazi inafanya ukaguzi wa mara kwa mara katika malango ya hifadhi na ofisi za mawakala wa utalii ili kujiridhisha kuwa muongozo huo unazingatiwa wakati wote.
“Changamoto zinazotokana na waajiriwa kutokulipwa kiwango stahiki, kuchelewa kulipwa au kutokulipwa kabisa zimekuwa zikishughulikiwa kwa karibu na Idara ya Kazi na vyama vya waongoza watalii na wapagazi,” amesema Dk. Ndumbaro.
Leave a comment