WAZIRI wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari nchini Tanzania, Dk. Ashatu Kijaji ameitaka menejimenti na watumishi wa wizara hiyo kufanya kazi kwa bidii na kwa kujituma ili kufikia malengo ya Serikali. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Dk. Kijaji ameyasema hayo jana Jumatatu, tarehe 14 Septemba 2021, katika kikao chake cha kwanza na menejimenti ya wizara hiyo kilichofanyika ofisi za wizara zilizopo Mtumba mara baada ya kuapishwa na Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, Ikulu ya Chamwino, Dodoma
Alisema, lengo na dhumuni la kuundwa kwa wizara hiyo ambayo sasa itaitwa wizara ya habari, mawasiliano na teknolojia ya habari ni kuwatumikia wananchi kwa kutekeleza kile kilichoelekezwa kwenye Ilani ya CCM ya 2020/25 kwa kuzisoma na kuziishi kurasa zinazohusu wizara hiyo.
Dk. Kijaji alisema watendaji wa wizara hiyo wanatakiwa kutekeleza wajibu wao kwa ufanisi mkubwa kwa kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi kwa sababu umma wa Watanzania una uchu wa kusikia kinachoendelea duniani hivyo kabla ya kufungia chombo chochote cha habari ni vema kutekeleza wajibu kwanza.
“Mifumo yote ya Taifa hili ipo chini ya wizara hii na tumeunganishwa na sekta ya habari, twendeni tukahakikishe tunafanya kazi kwa matokeo yanayoonekana,” alisema Dk. Kijaji.
Alisema matarajio yake ni kufanya kazi kwa ushirikiano mkubwa na upendo baina ya viongozi wa wizara hiyo bila kusuguana kwa kufuata utaratibu wa utumishi wa umma ikiwemo kutunza siri za Serikali na kutoa taarifa sahihi kwa umma.
Kwa upande wa naibu waziri wa wizara hiyo, Mhandisi Kundo Mathew alisema maelekezo aliyoyatoa Dk. Kijaji yamelenga kufanya kazi kwa matokeo yanayohitajikaili baadae yaoneshe mabadiliko katika jamii wanayoitumikia.
Dk. Kundo aliahidi yeye binafsi pamoja na menejimenti nzima ya wizara hiyo imepokea maelekezo hayo na inaenda kuyafanyia kazi kwa ufanisi mkubwa
Awali, Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Dk. Zainab Chaula aliitambulisha menejimenti ya wizara hiyo akiwemo Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa ambaye ni Mkurugenzi wa Idara ya Habari, Maelezo baada ya sekta ya habari kumegwa kutoka Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo na kuhamishiwa kwa iliyokuwa Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na kuunda Wizara mpya Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari.
Dk. Chaula alisisitiza menejimenti hiyo kuendelea kufanya kazi kwa kufuata sheria, taratibu na kanuni za utumishi wa umma ili matokeo ya kazi na majukumu ya kila mmoja wao iwe yenye tija na ufanisi mkubwa.
Naye Msemaji Mkuu wa Serikali na Mkurugenzi wa Idara ya Habari, MAELEZO, Gerson Msigwa kwa niaba ya menejimenti hiyo alisema wamepokea maelekezo ya waziri huyo na kuahidi watii, wasikivu na kuchapa kazi kwa kiwango ambacho kimetolewa muongozo na kiongozi huyo.
Leave a comment