DAKTARI Edward Hoseah, ameapishwa kuwa Rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), akimrithi Dk. Rugemeleza Nshala, aliyemaliza muda wake. Anaripoti Regina Mkonde, Arusha … (endelea).
Dk. Hoseah ameapishwa leo Jumamosi tarehe 17 Aprili 2021, na Corman Ngaro, Wakili Mwandamizi TLS, katika Ukumbi wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC), jijini Arusha.
Rais huyo mpya wa TLS, ameapishwa baada ya kushinda kiti cha Urais katika Uchaguzi Mkuu wa chama hicho, uliofanyika jana Ijumaa tarehe 16 Aprili 2021 katika Viwanja vya AICC.
Dk. Hoseah alishinda kwa kura 293 kati ya kura 802 zilizopigwa na mawakili walioshiriki uchaguzi huo.
Dk. Hoseah aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (Takukuru), aliwashinda wagombea wenzake wanne, Flaviana Charles (223), Francis Stolla (17), Shehzada Walli (192) na Albert Msando (69).
Mbali na uapisho wa Dk. Hoseah, Pia, Gloria Kabalamu, naye ameapishwa kuwa Makamu wa Rais wa TLS.
Wengine walioapishwa ni, Dk. Fauz Twaib na Rwekama Rweikiza, ambao wameapishwa kuwa viongozi wa Bodi ya Mali za TLS.
Naye Capt. Ibrahim Bendera, ameapishwa kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili ya Mawakili wa TLS.
Hali kadhalika, wajumbe wa Baraza la Uongozi la TLS nao pia waliapishwa.
Leave a comment