DAKTARI Edward Hoseah, ameibuka mshindi wa urais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS). Anaripoti Regina Mkonde, Arusha … (endelea).
Uchaguzi huo, umefanyika leo Ijumaa tarehe 16 Aprili 2021, katika ukumbi wa mikutano ya kimataifa wa Arusha (AICC).
Dk. Hoseah, aliyewahi kuwa mkurugenzi mkuu wa taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa (Takukuru) kati ya 2006-2015, amewashinda wenzake wanne, katika kinyang’anyiro hicho.
Akitangaza matokeo ya uchaguzi huo, Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi TLS, Wakili Charles Rwechungura, amesema Dk. Hoseah ameshinda kwa kura 293, kati ya kura 802 zilizopigwa na mawakili waliojitokeza.
Amesemq, Flaviana Charles amepata kura 223, huku aliyeshika nafasi ya tatu kwenye uchaguzi huo, Shehzada Walli akipata kura 192.
Rwechungura amesema, nafasi ya nne ni Albert Msando aliyepata kura 69 na wa mwisho Francis Stolla alipata kura 17.
Dk. Hoseah ataiongozo TLS kwa kipindi cha mwaka mmoja, kwa mujibu wa katiba ya chama hicho na baada ya kumalizika, akipenda kugombea tena, anaweza kufanya hivyo.
Anachukua nafasi iliyoachwa wazi na Dk. Rugemeleza Nshalla, ambaye amemaliza muda wake wa uongozi.
Baadhi ya marais waiowahi kuongoza TLs ni: Charles Rwechungura, Francis Stolla, Tundu Lissu, Fatma Karume na Dk. Rugemeleza Nshalla
Leave a comment