DAKTARI Edward Hoseah, Rais mpya wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), ameomba kukutana na Rais Samia Suluhu Hassan, ili kujadili namna ya kurekebisha sheria zinazokandamiza haki za binadamu na zinazompa mamlaka makubwa Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP). Anaripoti Regina Mkonde, Arusha … (endelea).
Dk. Hoseah ametoa ombi hilo, leo Jumamosi tarehe 17 Aprili 2021, baada ya kuapishwa kuwa Rais wa TLS, katika ukumbi wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC), jijini Arusha.
Ameapishwa baada ya kushinda kiti cha urais wa TLS, katika uchaguzi mkuu wa chama hicho, uliofanyika Ijumaa tarehe 16 Aprili 2021, jijini Arusha.
Dk. Hoseah amezitaja baadhi ya sheria kamdamizi ikiwemo Sheria ya Uhujumu Uchumi na Utakatishaji Fedha, zinazonyima dhamana kwa mahabusu wa makosa hayo.
“Nichukulie mfano, sheria ambazo zinatungwa na Bunge na kupitishwa zinazohusu bail (dhamana), mshtakiwa akishtakiwa uhujumu uchumi na utakatishaji fedha hapewi dhamana.”
“Haibishaniwi kwamba sheria hizi zinaondoa utu, dhamana ni utaratibu upo kwenye uendeshaji kesi za jinai kabla ya kesi kusikilizwa mahakamani,” amesema Dk. Hoseah.
Rais huyo mpya wa TLS amesema, “naomba Serikali yetu na naamini Serikali ya Mama Samia ni sikivu, tutakaa na wadau mbalimbali kuangalia sheria hizi kandamizi. Sababu mshtakiwa kukaa mahabusu muda mrefu kwa kweli ni kumnyima haki ya msingi.”
“Dhamana ni haki ya mtuhumiwa, ni pale tu kuna sababu za msingi zinapelekea kunyimwa dhamana na hii haki ya mahakama.”
Kuhusu sheria kumpa mamlaka makubwa DPP katika kesi, Dk. Hoseah amesema, kitendo hicho kinaondoa uhuru wa mahakama.
“Sheria nyingi zisimpe mamlalaka DPP, sababu ni sehemu ya washiriki wakati wa kuendesha mashtaka ya jinai. Inashangaza namna gani sheria inampa mamlaka makubwa kuiagiza mahakama. Mahakama ikiagizwa inaonekana hakuna uhuru wa mahakama,” amesema Dk. Hoseah.
Dk. Hoseah ameishauri, Serikali izingatie utawala wa sheria inapofanya maamuzi yake, ili kuondoa migogoro kwenye jamii.
“Serikali tunaisihi na kuiomba katika maamuzi wanayofanya wazingatie utu wa mtu na hili linaenda sambamba na waasisi wetu wa Afrika hasa Tanzania, Baba wa Taifa, Julius Nyerere katika maandishi yake amesisitiza utu, tukiitekeleza hii falsafa tuna amini migogoro mingi tunayoona kwenye jamii itapungua,” amesema Dk. Hoseah.
Amesema “Serikali ilitazame hili na mahakama itumie uwezo wake iliyopewa na katiba inayosema mahakama ina haki ya kuamua mgogoro wowote. Ni pendekezo letu kama uongozi mpya tuangalie athari ambazo wananchi wetu wa kawaida wana athiriwa na sheria kandamizi.”
Ombi hilo la Dk. Hoseah ni la kwanza tangu alipoingia madarakani kumrithi Dk. Rugemeleza Nshala aliyemaliza muda wake.
Dk. Hoseah ataiongoza TLS katika nafasi ya Urais kwa mwaka mmoja kuanzia Aprili 2021 hadi Aprili 2022.
Leave a comment