WAZIRI wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum imetambulishwa rasmi kwa jamii huku Waziri mwenye dhamana Dk. Dorothy Gwajima akijinadi kuwa ni kati ya wizara zitakazofanya vizuri. Anaripoti Danson Kaijage – Dodoma …(endelea)
Wizara hiyo mpya ambayo imetenganishwa na wizara ya afya inalenga zaidi kutoa huduma bora na muhimu kwa makundi yaliyotajwa kwa misingi thabiti na yenye tija kwa jamii.
Dk. Gwajima akizungumza na watumishi pamoja na wadau mbalimbali amesema kuwa wizara hiyo ipo tayari kutekeleza majukumu yake sambamba na maagizo mbalimbali yaliyotolewa na Rais Samia Suluhu Hassan katika kufikia azma yake ya kuwaletea wananchi maendeleo.
Dk. Gwajima ameitambulisha wizara hiyo rasmi jana tarehe 17 Januari, 2022 na kuwahakikishia Watanzania kuwa itafanya kazi kwa uweledi, umakini na kwa kasi ya ajabu.
Waziri Dk. Gwajima ameyasema hayo Jijini Dodoma kwenye Ofisi za Wizara zilizoko Mji wa Serikali, Mtumba wakati akizungumza na Menejimenti ya Wizara hiyo katika kikao cha kwanza kukutana tangu kuanzishwa kwa wizara hiyo mpya.
“Rais Samia ameona umuhimu wa kuwepo kwa Wizara hii ambayo ilikuwa hitaji muhimu katika utoaji huduma na kwa umuhimu huo itaweza kuratibu na kuhakikisha wananchi wa makundi yote wanashiriki kusukuma maendeleo ya Taifa kwa kupitia sekta husima,” alisema Dk. Gwajima.
Hatua hii inakuja baada ya Rais Samia kuanzisha Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum yenye lengo la kuhakikisha jamii inapata maendeleo na ustawi wao.
Leave a comment