KATIBU mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Dk. Bashiru Ally amewataka wavuja jasho wakiwemo wakulima kutokata tamaa au kuwa na tamaa ya mabadiliko ya haraka kwani kufanya hivyo kutawaingiza kwenye kupoteza kura zao na kukosa wanachokotaka kwa ajili ya maendeleo yao na nchi nzima kwa ujumla. Anaripoti Christina Haule, Morogoro … (endelea).
Dk. Ally alisema hayo jana wakati akizungumza kwenye mkutano mkuu wa Mtandao wa vikundi vya wakulima MVIWATA ambapo alisema, mkulima anayetaka mabadiliko lazima kura yake aipe thamani.
Aliwataja wavuja jasho hao kuwa ni pamoja na wafanyabiashara wadogo na wakulima wadogo ambapo alisema utegemezi wao utawaangusha.
Alisema, ni wakati sasa wakulima muda umefika wa kujitambua hasa katika suala zima la uchaguzi, kwani mtu anayetoa pesa akotaka kupata kura hataweza kumsaidia.
“Ukimuona mtu anatoa hela kuomba kura muogope, na kwa nini upokee hela ya mtu kama humpi kura!, huo ni unyonyaji,” alisema.
Hivyo aliwaasa wakulima kuacha utegemezi kwa wanasiasa wanaopenda vyeo, mali na siasa kwani hawataweza kuwatatulia matatizo yao kama wakulima na kubaki kujinufaisha wenyewe.
Alisema, demokrasia halisi kwa wavuja jasho ni uwezo wao katika uelewa wa mambo ikiwemo kiuchumi na kisaikolojia
Hivyo aliwashauri wakulima kujenga dhanaya kuendelezana kielimu ili waweze kuwapata viongozi wenye uwezo wa kuwaongoza wanaotoka ndani yao ambao wana uchungu na masuala yao.
Naye mkulima kutoka handeni Tanga Ramadhani Ally aliiomba Serikali kuangalia uezekano wa kutafuta suluhisho la ardhi yao ambayo imekufa kutokana na pembejeo za kilimo ikiwemo madawa, mbolea na mbegu.
“Mahindi tuliyolima msimu uliopita kwa kutumia mahindi ya dukani yameanza kuharibika ndani ya miezi mitatu tuu, huku ya mbegu za asili hayajaharibika, tunahitaji ardhi yetu irudishwe kuwa sawa,” alisema.
Leave a comment