DAKTARI Bashiru Ally, Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM), amevitaka vyama vya siasa nchini kutumia vyombo husika ikiwemo Baraza la Vyama vya Siasa, kumaliza tofauti zao. Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam … (endelea).
Dk. Bashiru ametoa wito huo leo tarehe 31 Machi 2020, katika mazishi ya Khalifa Suleyman Khalifa, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), katika makaburi ya Kisutu jijini Dar es Salaam.
Katibu huyo wa CCM amevitaka vyama hivyo kutumia baraza hilo, katika kufanya mazungumzo ya kumaliza tofauti zao.
“Na tutumie fursa zilizopo kama baraza la vyama vya siasa, ndio chombo chetu kikubwa sana ambacho tunaweza kuzungumza kumaliza tofauti zetu,” amesema Dk. Bashiru.
“Tunahimizwa kuwa na mshikamano wakati wote kutatua kero na shida za watu wetu. Tunashindana juu ya namna bora ya kutenda haki kwa watu,” amesema Dk. Bashiru.
Khalifa amefariki dunia usiku wa kuamkia leo katika Hospitali ya Aga Khan jijini Dar es Salaam, alikokuwa anapatiwa matibabu.
Akizungumzia kuhusu msiba huo, Dk. Bashiru ametoa salamu za rambi rambi za Rais John Magufuli kwa familia ya marehemu Khalifa.
Dk. Bashiru amesema Rais Magufuli atamkumbuka kwa mchango wake kwa taifa na ndani ya chama cha CUF.
“Nilikuwa Dodoma, nimepokea simu ya rais alfajiri. Sababu rais alijua ni alfajiri, alinitumia ujumbe ambapo nimeusoma, yeye anamtambua Khalifa kama rafiki yake, waliianza kazi ya uwakilishi mwaka 1995 pamoja.
Na waliendelea kuwa hivyo mpaka alivyofika daraja la juu la ukatibu mkuu wa CUF, yeye amesema anamjua kama mwenye upendo ujasiri na aliyetayari kutumikia wananchi, CUF imepoteza mtu muhimu sana. atakumbukuzwa kwa mchango wake,” amesema Dk. Bashiru kwa niaba ya Rais Magufuli.
Leave a comment