KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk Bashiru Ally, amepingana utamaduni ulioanza kujengwa ndani ya chama wa kupachika majina ya wagombea kwenye mashina mapya yanayofunguliwa. Anaripoti Hamis Mguta…(endelea).
Kiongozi huyo wa CCM amesema, majina ya mashina yanapaswa kubeba majina yenye ujumbe wa chama na serikali na si watu kama inavyojengeka sasa.
“Yanatakiwa majina yenye kubeba ujumbe wa chama na serikali,” amesema Dk. Bashiru na kuongeza “na sio majina ya wagombea.”
Dk. Bashiru ametoa kauli hiyo leo tarehe 1 Septemba 2019, akiwa kwenye ziara yake ya kichama katika jimbo la Kawe linaloongozwa na Halima Mdee wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).
Dk Bashiru alikuwa akizindua shina la Hapa Kazi Tu katika Kata ya Kawe, Dar es Salaam ambapo jina hilo ndio kauli mbiu ya Rais John Magufuli kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.
Katibu huyo wa CCM amekuwa akifanya ziara ya kuimarisha chama hicho huku kukiwa na malalamiko kutoka upinzani kwamba, Jeshi la Polisi linapendelea chama tawala huku upinzani ukinyimwa fursa hiyo.
Leave a comment