Friday , 29 March 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Dk 14 za Rais Mwinyi “nitashirikiana na kila mmoja”
Habari za Siasa

Dk 14 za Rais Mwinyi “nitashirikiana na kila mmoja”

Dk. Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar
Spread the love

RAIS mpya wa Zanzibar, Dk. Hussein Ali Mwinyi ametumia dakika 14 kutoa hotuba yake ya kwanza akiwa Rais wa visiwa hivyo huku akiahidi kuunda Serikali itakayokuwa uwazi, kuwajibika na usawa isiyokuwa na ubaguzi. Anaripoti Regina Mkonde …(endelea).

Pia, Rais Mwinyi amesema, yuko tayari kuendeleza maridhiano na mshikamano wa Wazanzibar ulioanzishwa na watangulizi wake akiwemo Dk. Ali Mamohed Shein, Rais mstaafu wa Zanzibar.

Rais Mwinyi, amesema hayo muda mfupi baada ya kuapishwa kuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar leo Jumatatu tarehe 2 Novemba 2020 katika Uwanja wa Aman visiwani humo.

Dk. Mwinyi ameapishwa na Jaji Mkuu wa Zanzibar, Othuman Ali Makungu kuwa Rais wa nane wa Zanzibar tangu kulipotokea mapinduzi visiwani humo tarehe 12 Januari 1964.

Rais Mwinyi alianza hotuba yake kwa saa 5:54 asubuhi na kuimaliza saa 6:10 mchana kwa kusema “Zanzibar oyeeeeee, Mapinduzi…” umati ukaitikia ‘daimaaaaaa’

Dk. Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar akiapishwa

“Nasimama mbele yenu kwa mara ya kwanza nikiwa Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Nimekula kiapo kuwa Rais wa nane wa Zanzibar,” amesema Rais Mwinyi huku akiibua shangwe uwanja mzima

Rais Mwinyi amesema, “namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya kuifikia leo, natambua wajibu ulioko mbele yangu wa kuwaongoza Wazanzibar bila kujali dini, ukabili au maeneo wanayotoka.”

Ametumia fursa hiyo, kusema Rais wa Tanzania John Pombe Magufuli, “alipenda kushiriki nasi leo lakini kwa sababu zilizoshindwa kuzuilika, ameshindwa kufika leo hapa na ameniagiza kuwafikishia salamu zake kwenu.”

Rais Magufuli amewashukuru Wazanzibar “kujitokeza kwa wingi kupiga kura na kuwachagua viongozi, kujitokeza kwa wingi tarehe 28 Oktoba 2020 ni ukomavu wenu kwamba uchaguzi ni njia sahihi ya kuwapata viongozi watakaoiongoza nchi hii kwa miaka mitano.”

Amesema, yeye pamoja na viongozi wengine waliochaguliwa, wajibu ulioko mbele yao ni kuwatumikia kwa uwezo wao wote ili kuifanya Zanzibar mpya yenye maendeleo kwa kila mmoja.

“Ninawapongeza na kuwashukuru sana wananchi kwa kusherekea ushindi kwa nidhamu na utulivu. Hongereni sana kwa hilo. Uchaguzi ni jambo la muhimu, kwani uchaguzi ni mchakato na amani ya kudumu ni msingi wa kudumu.”

“Nawapongeza wagombea wenzangu kwa nafasi ya urais kwa kuyapokea matokeo na kuyakubali na ninaahidi kushirikiana nao katika Serikali nitakayoiunda ili kujenga Zanzibar mpya,” amesema Rais Mwinyi aliyezaliwa tarehe 23 Desemba 1966.

Katika kusisitiza hilo, Rais Mwinyi amesema “lengo ni kuijenga Zanzibar, Zanzibar mpya itajengwa na wote na nitakuwa tayari kushirikiana kuijenga Zanzibar.”

Pia, ametumia dakika hizo 14, kutoa shukurani zake kwa chama chake cha mapinduzi kwa kumuamini na kumfanyia kampeni hadi akaibuka mshindi dhidi ya wagombea wenzake 16.

“Namshukuru Dk. Ali Mahomed Shein kwa kuniongoza na kunishauri na mimi sina cha kumlipa ila nitaenzi na kuendeleza pale alipoisha kwani uchaguzi sasa umeisha, kazi iliyoko mbele ni kushirikiana kuijenga Zanzibar yetu, kila mmoja ashiriki eneo alilopo,” amesema

Rais Mwinyi amesema, Serikali atakayoiunda itakuwa ya uwazi, uwajibikaji na usawa bila kubagua mtu kwa rangi au eneo analotoka ambayo itazingatia “nidhamu kwa watumishi, itakayokuwa na kasi kwa kuimalisha huduma za kijamii.”

Pia, amesema, takwira kamili ya Serikali atakayoiongoza, ataitoa hivi karibuni atakapokwenda kuzindua Baraza la Wawakilishi.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za SiasaMakala & Uchambuzi

Nani anasema kuna hasara ATCL?

Spread the loveRIPOTI za makusanyo na matumizi ya fedha katika Kampuni ya...

Habari za SiasaTangulizi

CAG: Wastaafu, wenza wao chanzo NHIF kufilisika

Spread the loveRIPOTI ya ukaguzi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu...

Habari za SiasaTangulizi

Vikundi hewa 851 vyalamba bilioni 2.6 mikopo ya halmashauri

Spread the loveVIKUNDI hewa vya wajasirimali wadogo 851 kutoka katika halmashauri 19...

Habari za SiasaTangulizi

Mashirika matano yapata hasara mabilioni ya fedha

Spread the loveMASHIRIKA matano ya Serikali yanayojiendesha kibiashara, yamepata hasara ya mabilioni...

error: Content is protected !!