DIWANI wa Kata ya Kawe, Mutta Rwakatare (CCM), aliyetoweka tangu Februari 2022, amepatikana akiwa katika hali ya ulevi kwenye nyumba ya rafiki wake wa kike aliyefahamika kwa jina la Ashura Matitu, maeneo ya Tabata, jijini Dar es Salaam. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumanne, tarehe 24 Mei 2022 na Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, ACP Jumanne Muliro, ikiwa imepita siku tano tangu Meya wa Manispaa ya Kinondoni, Songoro Mnyonge, kuliomba Jeshi la Polisi, limsake diwani huyo akidai alifichwa kusikojulikana.
“Jeshi la Polisi lilifanya ufuatiliaji wa taarifa hizo na kufanikiwa kumpata tarehe 23 Mei 2022, akiwa kwenye nyumba ya mwanamke mmoja aliyejulikana kwa jina la Ashura Ally Matitu, kabila la mzaramo, mkazi wa Tabata.
“Mwanamke huyo alidai diwani huyo ni rafiki yake wa siku nyingi kwa zaidi ya miaka 10 na alifika nyumbani kwake tarehe 19 Mei 2022, huku akiwa katika hali ya ulevi uliopindukia,” imesema taarifa ya Kamanda Muliro.
Taarifa ya Kamanda Muliro imesema, kutokana na diwani huyo ambaye ni mtoto wa marehemu Mchungaji Getrude Lwakatare, kukutwa katika mazingira ya ulevi, Jeshi la Polisi lilimkabidhi kwa ndugu zake kwa ajili ya matibabu.
“Kutokana na mazingira ya ulevi ambayo diwani huyo amekutwa nayo na maombi yaliyotolewa na ndugu zake kwa Polisi kwa ajili ya matibabu.
“Pia kutokana na kumbukumbu za nyuma, mwenendo na tabia za diwani huyo, Polisi limemkabidhi kwa ndugu zake kwa matibabu na tiba zaidi za kisaikolojia,” imesema taarifa ya Kamanda Muliro.
Leave a comment