MSANII wa muziki nchini Tanzania, Naseeb Abdul maarufu ‘Diamond Platnum’ amesema, kiwango cha fedha anachoingiza kwa mwezi, kutokana na mikataba mbalimbali ya kibiashara ni zaidi ya Sh. 200 milioni. Anaripoti Brightness Boaz, Dar es Salaam … (endelea).
Diamond amesema, kiwango hicho cha fedha ni hadi tarehe 23 Januari 2021 ambacho kinaweza kuongezeka kutokana na mikataba mingine atakayoingiza hivi karibuni na kampuni mbalimbali.
Amesema, fedha hizo anazozipata, ni tofauti na matamasha anayoyafanya pamoja na uwekezaji kwenye mambo mengine.
“Acha show zangu, uwekezaji wangu, endorsement zangu kwa mwezi naingiza Sh.222.6 milioni ambayo kwa wiki ni sawa na Sh.55.6 milioni, kwa siku Sh.7.9 milioni, kwa saa Sh.331,000 na kwa sekundi kama Sh.6,000,” amesema Diamond, leo Alhamisi tarehe 28 Januari 2021, alipokuwa akihojiwa katika kipindi cha The Switch, kinachorushwa na Wasafi FM.
Licha ya kushindwa kutaja moja kwa moja tahamani yake kwa sasa, Diamond amesema, “kuna wasanii wapo Nigeria wanajifanya wananizidi hela, nakwambia hawanizidi hela mimi kabisa na nikikwambia nawazidi nawazidi kweli.”
“Mimi mishahara na kodi ninayolipa kwa mwezi ni hela kubwa, najivunia kuwa Mtanzania ninayelipa kodi,” amesema.
Amesema, mwaka jana, aliutumia sana kufanya uwekezaji na ndiyo maana ulipoibuka ugonjwa wa coronam yeye hakuteteleka na kutokana na uwekezaji huo, umefanikisha tamasha la tumewasha, lililofanyika mikoa mbalimbali, kufanyika bure.
“Tamasha moja la Tumewasha, tunatumia kama milioni 100 na watu wanaingia bure. Hii inatokana na uwekezaji mkubwa nilioufanya mwaka jana na ndiyo maana hata corona ilipokuja sikuwa na wasiwasi,” amesema Diamond ambaye amedokeza mwaka huu atautumia kujitambulisha zaidi yeye binafasi, kama kimavazi na nyumba yake ya kuishi
Na kodi analipa kiasi gani? TRA mpooooooo????