MSANII wa muziki nchini Tanzania, Diamond Platinum ametumia jukwaa la burudani kuwasisitiza wananchi wa Taifa hilo, kujiandaa kuandikishwa katika sensa ya watu na makazi itakayofanyika Agosti 2022. Anaripoti Matilda Buguye, Dar es Salaam … (endelea).
Diamond ametoa nasaha hizo leo Jumatatu, tarehe 14 Septemba 2021, katika Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma, kwenye hafla ya uzinduzi wa kitabu cha mkakati wa uelimishaji na uhamasishaji wa sensa hiyo.
Kabla ya kuanza kutoa burudani kwa wananchi na viongozi mbalimbali akiwemo Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, Diamond amesema “…jamani tulieni kwanza, Sensa ni maendeleo na lazima ujiandae kuhesabiwa.”
Huku mamia ya wananchi wakisubiri aanze kutumbuiza, Diamond akasema “lazima tujiandae kuhesabiwa na unapohesabiwa unaisaidia serikali kupanga mipango yake.”
Mara baada ya kumaliza kutoa nasaha hizo, Diamond akiwa na kikundi chake cha burudani, wakaanza kuwatumbuiza kwa nyimbo mbalimbali hali iliyoibua shangwe uwanjani hapo.
Wakati Diamond akiendelea kumwaga burudani na shangwe zikitawala, mgeni rasmi kwenye shughuli hiyo, Rais Samia aliondoka akimwacha mzaliwa huyo wa Tandale, jijini Dar es Salaam, akiwaburudisha.
Ilikuwa ni mara ya pili anapanda jukwaani akitangulia awali kupandishwa na kuimba wimbo mmoja wa ‘Baba Lao’ ambao alitumia takribani dakika nne kuwaburudisha wananchi na viongozi akiwemo Rais Samia.
Nyakati zote alizopanda jukwaani na wakati mwingine kushuka jukwaani na kusogea karibu na wananchi na kuanza kuimba nao, Diamond alionekana kuzikonga nyoyo za wananchi hao.
Awali, Mkurugenzi Mkuu wa ofisi ya Takwimu Tanzania (NBS), Dk. Albina Chuwa alisema, sensa hiyo itakayofanyika Agosti mwaka 2022, ni ya tofauti na sensa tano zilizopita kwani itakuwa ya kidijitali.
Leave a comment