DENI la Taifa la Tanzania, limeongezeka kwa Sh. 5.4 trilioni, kutoka Sh. 55.5 Aprili 2020, hadi kufikia Sh. 60.9 trilioni, Aprili 2021. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Alhamisi, tarehe 10 Juni 2021 na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Mwigulu Nchemba, akiwasilisha taarifa ya hali ya uchumi wa Taifa kwa 2020, bungeni jijini Dodoma.
Dk. Mwigulu amesema, katika deni hilo, la nje ni Sh. 43.7 trilioni, huku la ndani likiwa ni Sh. 17.3 trilioni.
“Hadi Aprili 2021, deni la Serikali lilikuwa Sh. 60.9 trilioni, ikilinganishwa na Sh. 55.5 trilioni, kipindi kama hicho mwaka 2020. Kati ya kiasi hicho, deni la nje ni Sh. 43.7 trilioni na deni la ndani ni Sh. 17.3 trilioni,” amesema Dk. Mwigulu.
Waziri huyo wa fedha amesema, ongezeko hilo limesababishwa na mikopo ya nje ya nchi, ambapo Serikali ilikopa kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo.
“Ongezeko hilo lilitokana na kupokelewa kwa fedha za mikopo mipya, kwa ajili ya kugharamia miradi ya maendeleo,” amesema Dk. Mwigulu.
Hata hivyo, Dk. Mwigulu amesema, deni hilo ni himilivu, katika vipindi vyote.
“Taarifa ya tathmini ya uhimilivu wa deni iliyofanyika Desemba 2020, inaonesha kuwa deni la Serikali ni himilivu katika kipindi cha muda mfupi, wa kati na mrefu. Kwa kuzingatia ukomo wa viashiria vyote vinavyokubalika kimataifa,” amesema Dk. Mpango.
Miongoni mwa miradi ya ujenzi wa miundombinu ambayo Serikali ya Tanzania inajenga kwa kutumia fedha za mikopo, ni ujenzi wa Reli ya Kiwango cha Kimataifa (SGR), kutoka Morogoro hadi Makutupora mkoani Dodoma.
Ambapo imekopa Sh. 3.3 trilioni kutoka Benki ya Standard Chartered Group.
Asante mwigilu tunasubiri vitendo na matendo ahadi ni deni