BENKI ya NMB nchini Tanzania imetoa vifaa mbalimbali vya shule za msingi, sekondari pamoja sekta ya afya vyenye thamani ya Sh.27 milioni kwa Wilaya ya Ubungo jijini Dar es Salaam. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Meneja wa Benki ya NMB Kanda ya Dar es Salaam, Donatus Richard alisema wamekabidhi vitanda kumi vya kulazia wagonjwa, vitanda vitano vya kujifungulia, mashine 15 za kupimia presha na mapazia 10 ya kutenganisha wodi.
Kwa upande wa shule ya msingi Kwembe walipata viti na meza 35 za walimu huku shule ya Urafiki wakipata meza na viti 110 kwajili ya wanafunzi.
“Jumla ya vifaa hivi tunavyokabidhi leo ni muendelezo wa ushirikiano mwema kati yetu na Wilaya ya Ubungo na ndio maana tulipopata maombi haya, tulifarijika na kuamua mara moja kushiriki katika kuchangia sekta ya elimu na afya kwa wilaya hii,” alisema Donatus.
Meneja huyo alisema mbali na mengi yanayofanywa na Serikali kwaajili ya wananchi, wao kama wadau wa maendeleo wanao wajibu wa kuendelea kuchangia katika jamii kwani jamii hizo ndio chanzo cha mafanikio mengi ambayo benki hiyo imekuwa ikiyapata.
“Jamii hizi ndio chanzo cha mafanikio yote ambayo benki ya NMB inapata hata kuwa benki kinara zaidi hapa nchini. Na ndio maana kurejesha sehemu ya faida yetu kwa jamii yetu imekuwa kawaida yetu kwani tunathamini sana jamii zetu na tunaamini ustawi kwa jamii zetu ndio ustawi wa Benki yetu pia,” alisema.
Akizungumza wakati wa kupokea vifaa hivyo, Mkuu wa Wilaya ya Ubungo (DC), Kheri James alisema Benki ya NMB inastahili pongezi kwani wamekuwa karibu sana sio tu kwa wilaya ya Ubungo bali kwa wilaya mbalimbali nchini na wamekuwa wakisaidia sana hususani katika sekta ya elimu na Afya.
“Mimi niwapongeze sio tu kwa misaada yenu mnaotusaidia mara kwa mara lakini pia kwa kutupa misaada hii katika muda muafka na katika kipindi ambacho tunaihitaji sana misaada hii.”
“Hospitali hii ya wilaya ndio imeanza hivyo vifaa hivi vitakuwa ni vya muhimu sana kwani Serikali imeshakamilisha ujenzi na sasa wananchi wa Ubungo watahudumiwa vyema katika kituo hiki,” alisema James.
“Nitoe wito wangu kwa watumishi wa hospitali hii na waalimu wa shule zinazopokea vifaa hivi, vifaa hivi vikawe chachu ya maendeleo ya sekta hizi. Tuvitumie vyema kwa maslahi mapana ya wananchi tunaowahudumia ili kila akifika kupata huduma akute vifaa hivi vikiwa katika hali nzuri na vitunufaishe,” alisema.
Mkuu huyo wa wilaya aliwaoamba Benki ya NMB wasiache kuendeleza kuisaidia wilaya hiyo kwani bado zipo sehemu ambazo bado zinakumbwa na changamoto Mbalimbali lakini pia akitumia fursa hiyo kualika wadau wengine waige mfano wa Benki ya NMB.
Akizungumza kwa niaba ya wananchi wa Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo, Meya wa Manispaa ya Ubungo, Jaffari Juma Nyaigesha aliishukuru Benki ya NMB huku akiwaasa wananchi wawe chachu ya kuhakikisha misaada hii inatumika vyema na inatunzwa katika hali nzuri ili iwanufaishe wengi zaidi.
Kwa upande wake, Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya wilaya ya Ubungo, Dk. Imani Mwanang’ombe amesema kwa misaada huo kutoka Benki ya NMB, hospitali ya wilaya ya Ubungo itakuwa na uwezo wa kuhudumia wagonjwa zaidi ya 250 kwa wiki hivyo kusababisha kuhudumia wananchi zaidi ya 1000 kwa mwezi huku idadi hiyo ikitatazamiwa kuongezeka baada ya kukamilisha majengo mengine ya hospitali hiyo mnamo mwezi wa nane mwaka huu.
Leave a comment