MWALIMU Mohamed Utaly, Mkuu wa Wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro, amewataka wavunaji wa misitu, wabebaji na wauzaji wa mkaa kwenye pikipiki na fuso kukata vibali. Anaripoti Christina Haule, Mvomero … (endelea).
Amesema, vibali hivyo vya uvunaji misitu, vinatolewa na Wakala wa Misitu Tanzania (TFS), na kwamba hatua hiyo itaepusha uvunaji holela unaosababisha uharibifu wa mazingira nchini.
Mwalimu Utaly ametoa kauli hiyo leo tarehe 6 Novemba 2019, wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake.
Amesema, kitendo cha wauzaji hao wa mkaa kubeba magunia zaidi ya moja kwenye pikipiki, ni hatari kwao na pia kinaashiria uharibifu wa misitu na mazingira kwa ujumla.
Amesema, tayari Halmashauri ya wilaya hiyo, imeanza kudhibiti suala hilo kwa kutoa elimu kwao sambamba na kuwakamata wanapokutwa njiani.
Pia, TFS inawataka wakulima wanaokata sehemu ya msitu kwenye mashamba yao kwa ajili ya kujiandaa na msimu, kuhakikisha wanakuwa na vibali vitavyowaruhusu kufanya hivyo.
Ofisa Uraghibishi wa MJUMITA, Elida Fundi amesema, mradi wa mkaa endelevu unaofadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Uswis (SDC), umeweza kutoa elimu kwa wananchi wa vijiji vitano vya awali na vitano vipya wilayani humo.
Vijiji hivyo vya mradi huo wilayani Mvomero ni pamoja na Maharaka, Kihondo, Sewekipera, Msongozi, Kisengele, Msolokelo, Ndole, Machimba, Magunga na Diburuma.
Leave a comment