JOKATE Mwengelo, Mkuu wa Wilaya ya Temeke (DC) Mkoa wa Dar es Salaam, nchini Tanzania amewaomba wanaume kuwaunga mkono wanawake ili kushinda nafasi ya urais mwaka 2025. Anaripoti Patricia Kighono, TUDARCo … (endelea).
DC Jokate amesema, uchaguzi mkuu ujao 2025 ni kwa kwenda kumweka mwamake madarakani.
Ametoa kauli hiyo leo Jumatano, tarehe 15 Septemba 2021, saa chache kupita tangu Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan kuwataka wanawake nchini humo, kuweka mipango vizuri ili katika uchaguzi huo wamuweka rais mwanamke madarakani.
Rais Samia amesema, nafasi aliyonayo sasa ni kwa kudra za Mwenyezi Mungu.
Ni baada ya kifo cha aliyekuwa Rais John Magufuli, kilichotokea tarehe 17 Machi 2021 na kwa mujibu wa Katiba, Samia aliyekuwa makamu wa Rais kuapishwa kuwa Rais.
“Niwaambie wanawake bado hatujaweka rais mwanamke madarakani, amekaa kwa sababu ya kudra za Mwenyezi Mungu na matakwa ya Kikatiba. Rais mwanamke tutamuweka mwaka 2025,” amesema Rais Samia
Mara baada ya kauli hiyo, DC Jokate ameandika katika ukurasa wake wa Twitter akisema “ni kweli kabisa 2025 ni mwaka wa kumuweka Rais Mwanamke Ikulu.”
“Ni wakati sasa wa wanawake wote kuungana na kutumia fursa hii kufanikisha hili na kuendelea kuandika historia Tanzania, naamini wanaume pia watatuunga mkono maana nia ya Mama kulitumikia Taifa letu wote tumeiona,” amesema Jokate ambaye amewahi kuwa Miss Temeke.
“Lakini pia kwa kutambua wanawake tumefanya kazi kubwa kuleta uhuru wa nchi yetu, kujenga siasa za nchi yetu. Na pia Kama Mhe Rais alivyosema tumekuwa chachu nyuma ya wanaume wengi kupata vyeo vya juu. Ni wakati wetu sasa!!! Namuunga mkono Mama, 2025 twende na Mam.”
Jokate amehitimisha kwa kusema “#MamaKasema 2025 Mungu akijalia Wanawake Tutaweka Rais wa Kwanza Mwanamke Tanzania.”
Leave a comment