MKUU wa Wilaya ya Dodoma, Shekimweri Jabiri amewataka wazazi na walezi kuhakikisha wanapeleka watoto wao shule hususani walioshindwa kuendelea na masomo. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Mkuu wa wilaya hiyo ametoa kauli hiyo leo tarehe 8 Septemba, 2022 kwenye kilele cha maadhimisho ya wiki ya elimu ya watu wazima iliyofanyika katika uwanja wa sanamu ya kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere jijini Dodoma.
Shekimweri amesema kuwa wapo baadhi ya watoto wengi ambao wameshindwa kuendelea na masomo na wengine kukataliwa na mfumo wa kujiunga na elimu ya msingi au sekondari lakini kwa sasa kwa kutumia mfumo wa elimu ya watu wazima wanahaki ya kuendelea na masomo.
“Ukitaka kuendelea kutawala watu, kuwaonea watu na kushindwa kuwapatia huduma muhimu na wasilalamike… wanyime elimu.
“Lakini kwa kuliona hilo Rais Samia Suluhu Hassan ametoa maelekezo kuwa watoto wote ambao waliokatisha masomo yao iwe kwa bahati mbaya au kwa changamoto yoyote ya kimaisha basi anayo fursa ya kuendelea na masomo sasa” ameeleza Shekimweri.
Aidha, amesema kitendo cha kumnyima mtu yoyote elimu ni kitendo cha kumtengenezea umasikini kwani hata maandiko matakatifu yanahimiza kuishika sana elimu.
Pamoja na hayo Mkuu huyo wa wilaya amesema kwa wilaya ya Dodoma sasa imefanikiwa kuwapatia elimu wanafunzi 50 waliokatisha masomo kwa sababu mbalimbali jambo ambalo amesema ni maendeleo lakini bado jitihada kubwa za kuwapata wengine zinaendelea.
“Wapo watoto wengi walioshindwa kuendelea na masomo kwa sababu mbalimbali, wengine walibakwa, wengine uchumi na wengine ni changamoto ya ujana balehe.
” Kwa maana hiyo watu wa elimu wanatakiwa kuendelea kutafuta uwezekano wa kuwapata watoto ambao wanahitaji kuendelea na masomo kwa lengo la kujiendeleza,” ameeleza Shekimweri.
Leave a comment