MAMLAKA ya Majisafi na Ufasi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) imekabidhiwa Miche ya Michikichi 30,000 kutoka kwa Wakala wa Mbegu za Kilimo (ASA) katika Shamba la Wakala Mwele Tanga. Anaripoti Mwandishi Wetu, Pwani … (endelea).
Miche hiyo itapandwa pembezoni mwa Mto Ruvu ambapo itatunzwa kwa kushirikiana na wananchi waishio pembezoni mwa vyanzo vya maji.
Makabidhiano hayo, yamefanyika hivi karibuni kati ya ASA na DAWASA.
Mkuu wa kitengo Cha Mazingira wa DAWASA, Mhandisi Modester Mushi alisema miche hiyo itatumika katika kulinda na kutunza vyanzo vya maji katika Mto Ruvu.
Alisema DAWASA inatambua mpango wa serikali wa kukabiliana na changamoto ya upungufu wa mafuta ya kula nchini ndio maana ikaamua kupanda miche hiyo ya michikichi kwa kuunga juhudi za serikali za kupata mafuta.
Mhandisi Modester alisema michikichi hiyo itakuwa ni mali ya wananchi ikiwapatia kipato kwa kupata mafuta huku ikitunza mazingira kwani ni miti yenye urafiki na mazingira.
Alisema mamlaka hiyo imejipanga kuhakikisha inakabiliana na uharibifu wa mazingira kwa kutoa elimu kwa wananchi ikiwa na kupanda miche hiyo ambapo itaanza kupandwa katika Mto Ruvu ambao hutoa maji asilimia 92 kwa mikoa ya Dar es Salaam na Pwani kutoka katika mtambo wa maji Ruvu chini uliopo Bagamoyo na Ruvu juu uliopo Mlandizi.
Alisema kwa kushirikiana na Ofisi ya Bonde la Wami/Ruvu wanatarajia kupanda hadi vyanzo vikuu vya Maji vya Milima ya Uluguru Mkoani Morogoro ambapo ni zaidi ya kilomita 200. Kwa sasa wanatarajia kupanda Miche hiyo zaidi ya kilomita 40 kuanzia Bagamoyo katika Mtambo wa maji wa Ruvu chini.
Aliipongeza Wakala wa Mbegu za Kilimo (ASA) kwa kutoa Miche hiyo bure na bila kusita Mara baada ya kuomba maombi na yakajibiwa kwa haraka na hatimaye kukabidhiwa Miche hiyo 30,000.
Akikabidhi Miche hiyo Mkuu wa wilaya ya Mkinga, Kanali Maulidi Surumbu aliitaka DAWASA kuhakikisha wanaitunza na kuifuatilia miche hiyo ili iweze kutoa matokeo kama wanayotarajia.
Alisema DAWASA wametazama kichikichi kwa jicho la tatu la kutatua changamoto ya mafuta na kuongeza uchumi kwa wananchi kupitia mafuta watakayo kuwa wakibangua ambapo inaelezwa Michikichi huvunwa Mara nne kwa mwaka.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Mazao wa Wakala wa Mbegu za kilimo ASA, Dk. Justine Ringo akikabidhi miche hiyo kwa Mkuu wa wilaya ya Mkinga kabla ya kukabidhiwa kwa DAWASA alisema ASA mkakati wao nikuzalisha miche mingi zaidi ili kutatua tatizo la mafuta nchini.
Aliwapongeza DAWASA kwa kuona umuhimu wa kuwa na mradi huu wa Michikichi ambayo ni rafiki wa mazingira lakini pia itasaidia kupunguza tatzo la Mafuta kwa wakazi wa maeneo hayo.
Alisema ASA hadi sasa imekwisha toa Miche zaidi ya 500,000 huku uzalishaji wa miche hiyo ukiendelea.
Ringo alizitaka taasisi nyingine kujitokeza kuchukua miche ya michikichi kwa Wakala wa Mbegu za kilimo ASA ilikuunga mkono serikali kwa kukabiliana na tatizo la mafuta.
Leave a comment