DAKTARI wa aliyewahi kuwa Waziri wa Mambo ya Nje nchini Bernard Membe, ameondoa utata kuhusu ya kifo cha mwanasiasa huyo mkongwe na kusema hajauawa bali kifo chake kimetokana na maambukizi ya ghafla ya mapafu yaliyopelekea damu kuganda. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam …(endelea).
Daktari huyo binafsi wa Benard Membe, Profesa Harun Nyagori ametoa kauli hiyo leo tarehe 12 Mei 2023 na kusisitiza kuwa kifo cha mwanasiasa huyo kimechangiwa na ugonjwa wa maambukizi ya mfumo wa mapafu hewa.
Kauli ya daktari huyo imekuja baada ya kuibuka taarifa mbalimbali katika mitandao ya kijamii kuhusu chanzo cha kifo chake na kuibua utata.
Membe amefariki dunia leo tarehe 12 Mei 2023 katika Hospitali ya Hubert Kairuki jijini Dar es Salaam baada ya kukimbizwa hospitali hapo saa 12 asubuhi na wanafamilia hali yake ilipobadilika ghafla.
Akizungumza nyumbani kwa marehemu, Profesa Harun amesema ugonjwa huo unasababisha mgando wa damu na kuzuia mapafu kupeleka hewa ya oksijeni.
“Hali hii inaweza kumkuta mtu yeyote mara tu anapopata maambukizi haya kwa njia ya hewa hata kwa wagonjwa wanaopata pneumonia pia inaweza kuwakuta.
“Kinachozungumzwa huko mtaani kwamba mzee ameuawa amepewa sumu sijui nini, hiyo iondoke, ukweli ni kwamba amefariki kwa maradhi ya kawaida,” amesema Profesa Nyagori ambaye pia ni Mtaalamu wa Magonjwa ya Moyo kutoka Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI).
Aidha, amesema ugonjwa huo hakuwa nao muda mrefu, ulimuanza siku tatu zilizopita kwa homa na kifua, lakini juzi ndiyo ulizidi.
Leave a comment