WAZIRI Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa ameshiriki mazishi ya Mary Ndugai, dada wa Spika wa Bunge, Job Ndugai. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mpwapwa … (endelea).
Mary alifariki dunia Jumamosi iliyopita ya tarehe 23 Januari 2021, wilayani Mpwapwa mkoani Dodoma.
Mazishi hayo ya Mary yamefanyika leo Jumatatu, 25 Januari 2021, katika makaburi ya Ving’awe wilayani Mpwapwa mkoani Dodoma na kuhudhuliwa na viongozi mbalimbali wa Serikali na Bunge.
Akizungumza baada ibada ya kumuombea marehemu Mary iliyofanyika katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) jimbo la Mpwapwa, Waziri Mkuu, Majaliwa amewaomba wafiwa wawe na subira na utulivu katika kipindi hiki kigumu.
“Nimekuja kuungana nanyi kwa niaba ya Mheshimiwa Rais John Magufuli na Makamu wa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan kutoa pole kwa Mheshimiwa Spika Job Ndugai kufuatia msiba mzito wa kuondokewa na dada yake mpendwa Mary.”
Waziri Mkuu amesema, msiba huo ni mzito na jukumu kubwa ni kumuomba Mwenyezi Mungu ailaze roho ya marehemu pahala pema, hivyo amewaomba watoto wa marehemu, ndugu na jamaa wawe watulivu katika kipindi hiki kigumu cha majonzi.
Kwa upande wake, Spika wa Bunge, Job Ndugai amewashukuru viongozi wa dini, Serikali na waombolezaji kwa kujitokeza na kuifariji familia kufuatia msiba huo.
Pia, amewashukuru madaktari na wauguzi wa Hospitali ya wilaya ya Mpwapwa ambapo marehemu alikuwa akitibiwa.
Viongozi wengine waliohudhuria mazishi hayo ni Naibu Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson, Waziri wa Mambo ya Ndani, George Simbachawene, Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Mwigulu Nchemba, Katibu wa Bunge, Stephen Kigaigai na baadhi ya wabunge.
Leave a comment