CHAMA cha Walimu Chamwino mkoani Dodoma (CWT) kimelalamikia walimu kufanyishwa kazi siku za mapumziko ya mwisho wa wiki bila malipo. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Pia kimeeleza kuwa, walimu hao hawapewi chakula kinyume na kanuni na miongozo ya kazi kwa mujibu wa sheria ya ajira na mahusiano kazini.
Malalamiko hayo yametolewa leo tarehe 18 Februari 2019 na Clement Mahemba, Mwenyekiti wa CWT wilaya hiyo wakati alipozungumza na waandishi wa habari wilayani hapo.
Mahemba amedai, utaratibu huo ambao umeandaliwa na Ofisa Elimu Msingi wilayani hapo umekuwa ukinyanyasa walimu kutokana na kuwatumikisha siku za mapumziko ambazo ni Jumamosi na Jumapili.
Amedai, pamoja na walimu hao kutumikishwa kazi katika siku za kwenda kufanya ibada lakini pia katika mpango huo ambao ofisa elimu huyo anauita kuwa ni vikao kazi, kumekuwa hakuna malipo yoyote wala chakula.
“Walimu wanafanyishwa kazi siku za Jumamosi pamoja na Jumapili siku ambazo wengi wao wanatakiwa kufanya mapumziko kwa jili ya kujiandaa Jumatatu kwenda kufundisha,” amesema na kuongeza;
“Lakini pia walimu hawa wanatoka umbali mrefu kuna walimu wanatoka Kijiji cha Champumba kwenda Mlowa barabarani ni zaidi ya kilomita 80 kwenda kushiriki vikao kazi hivyo n ahata kukosa muda wa kufanya maandalizi ya Jumatatu.”
Mahemba amesema, kitendo cha mwajiri kumwita mtumishi wake kazini siku za mapumziko anatakiwa kumlipa kama ambavyo sheria ya ajira na mahusiano kazini namba 6 ya mwaka 2004 kifungu cha 24(1)6 na 24(4) vinavyoelekeza.
Akijibu malalamiko hayo Athumani Massasi, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Chamwino amesema, anachofahamu ni kuwa, hakuna mwalimu aliyelazimishwa na kwamba, wote wanafanya hivyo kwa utayari wao.
“Ninacho kifahamu mimi mwandishi, hawa walimu ni makubalianao yao hivyo hakuna mwalimu yeyote ambaye amelazimishwa kufanya hivyo wanavyofanya sasa lakini kama unataka kufahamu zaidi njoo ofisini,” amesema.
Leave a comment