MBUNGE wa Malindi Visiwani Zanzibar, Ali Salehe (CUF) amedai kuwa, kuna mkakati wa kuzuia baadhi ya wananchi katika kujiandikisha kwenye usajili wa vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Salehe alitoa madai hayo jana tarehe 4 Oktoba 2018 wakati akizungumza na wanahabari, ambapo aliihusisha hatua hiyo na mkakati wa kisiasa kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2020.
Alidai kuwa, kitendo hicho ni miongoni mwa figisu zinazoandaliwa na wanasiasa na kuitaka serikali kuingilia kati suala hilo.
Wakizungumza katika nyakati tofauti baadhi ya wakazi wa jimbo hilo, walidai kuwa, wamekuwa wakikumbana na masharti magumu pindi wanapokwenda kujisajili huku baadhi yao wakieleza kuwa, baadhi ya wahusika wamekuwa wakihitaji kiasi cha fedha ndipo wafanye usajili.
Akizungumzia kuhusu sakata hilo, Dk. Hussein Shabaan, Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Usajili wa Matokeo ya Kijamii Zanzibar, alilaani figisu hizo akisema kila Mzanzibar mwenye sifa stahiki anatakiwa kupata kitambulisho, na kuwataka wahusika kutoa kitambulisho hicho pasina ubaguzi.
Dk. Shaaban alisisitiza kuwa, ili mwananchi apate kitambulisho anatakiwa kuwa na cheti cha kuzaliwa pamoja na barua kutoka kwa sheha wa shehia husika.
Leave a comment