CHAMA cha Wananchi (CUF), kimetangaza kusimama peke yake katika Uchaguzi Mkuu unaotarajia kufanyika Oktoba mwaka huu. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 27 Januari 2020, na Prof. Ibrahim Lipumba, mwenyekiti wa chama hicho wakati akizungumza katika kongamano la kuwakumbuka wafuasi wa CUF, waliopoteza maisha katika maandamano ya tarehe 27 Januari 2001 visiwani Zanzibar.
Prof. Lipumba amesema, Baraza Kuu la Uongozi wa CUF limeagiza chama hicho limeazimia kusimamisha mgombea wake wa uchaguzi, wagombe wa ubunge na udiwani nchi nzima, pasina kushirikiana na chama chochote.
“Sisi tutaweka mgombea urais, wabunge na madiwani nchi nzima. Tunachohitaji kuwa na uchaguzi ulio huru na haki ili wapiga kura kauli yao iheshimiwe,” amesema Prof. Lipumba.
Wakati huo huo, Prof. Lipumba amemuomba Rais Magufuli kuweka uwanja wa siasa ulio sawa kwa vyama vyote, ili kujenga mazingira ya uchaguzi huo kuwa huru na wa haki.
“Na wito wangu kwa Rais Magufuli sisi tunatambau wewe ndio rais una dhamana ya kujenga mazingira ya kuendeleza demokrasi. Vyama vya siasa wapewe uhuru wa kufanya shughuli zao, polisi wasipoteze muda kufuatilia vyama vya siasa,” amesema Prof. Lipumba na kuongeza;
“Rais Magufuli jenga uwanja wa kisiasa ulio sawa pamoja na mapungufu ya sheria ya vyama vya siasa. Lakini sheria ya vyama vya siasa imetoa ruhusa kufanya siasa.”
Prof. Lipumba amesema “Tunahitaji uchaguzi 2020 usiwe chanzo cha madhara uwe eneo la kuendeleza amani.”
Leave a comment