Friday , 19 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa CUF yaomba kodi mitandao ya simu ifutwe
Habari za Siasa

CUF yaomba kodi mitandao ya simu ifutwe

Mhandisi Mohammed Ngulangwa, Mkurugenzi wa Habari -CUF
Spread the love

CHAMA cha Wananchi (CUF), kimeiomba Serikali ifute kodi ya mitandao ya simu, kwa maelezo kwamba inaumiza wananchi, hasa wa kipato cha chini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).

Wito huo umetolewa leo Alhamisi, tarehe 15 Julai 2021 na Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Mahusiano na Umma CUF, Mhandisi Mohamed Ngulangwa.

Kodi hiyo iliyopewa jina la ‘Mshikamano’,  imeanza kutozwa leo, baada ya kupitishwa na Bunge la Bajeti, lililohitimisha shughuli zake hivi karibuni.

Kwa mujibu wa kodi hiyo ya miamala ya simu, mtumiaji anatozwa kuanzia Sh. 10 hadi 10,000,  katika muamala wa kutuma au kutoa pesa, kulingana na thamani ya muamala wa fedha husika.

Mkurugenzi huyo wa habari CUF, amemuomba Rais Samia Suluhu Hassan, akutane na viongozi wa vyama vya siasa, ili wampe mbinu sahihi ya kukuza uchumi bila kuumiza wananchi.

“Hii tozo inapaswa kufutwa mara moja na Rais Samia , anapaswa kutumia Kikao  chake na viongozi wa vyama vya siasa kujifunza kutoka CUF,  namna sahihi na isiyoumiza katika kuikwamua Tanzania Kiuchumi,” amesema Mhandisi Ngulangwa.

Mhandisi Ngulangwa amesema kodi hiyo itawaathiri wafanyabiashara hasa wadogo.

“Wananchi wamekuwa wakitegemea mitandao ya simu kufanya miamala mbalimbali ya kufanikisha biashara zao. Kuna wanaofanya biashara za mazao ya shambani na biashara zingine, ambao wamekuwa wakikamilisha biashara hizo kupitia miamala ya simu,” amesema Ngulangwa na kuongeza:

“Hili lilitegemewa sana katika kukuza biashara hizi, ambazo faida zake ni ndogo sana. Leo gharama ya kutuma milioni moja kwa mkulima  Morogoro ni takribani mara mbili ya gharama ya nauli ya kwenda na kurudi baina ya Morogoro na Dar es Salaam.”

Serikali ya Tanzania inatarajia kutumia zaidi ya Sh. 600 bilioni, fedha zitakazotokana na kodi hiyo kwa mwaka wa fedha wa 2021/22, kwa ajili ya utekelezaji miradi ya elimu, afya ya msingi na miundombinu ya barabara.

Kwa mujibu wa Waziri Ofisi ya Rais-Tamisemi, Ummy Mwalimu, fedha hizo zitatumika kujenga  vyumba vya madarasa zaidi ya 10,000, maabara za sayansi za shule za sekondari 1,043, shule za kata 300 na shule za sayansi za sekondari za wasichana 10.

Pia, zitatumika kujenga zahanati 756 na kukamilisha maboma ya zahanati 900, pamoja na kununua vifaa tiba.

Kwa upande wa miundombinu, fedha hizo zinatarajia kujenga barabara za kiwango cha lami zenye urefu wa kilomita 250, kupandisha hadhi barabara za udongo kuwa changarawe urefu wa kilomita 5,834 na madaraja makubwa 64.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

Tume huru ya uchaguzi yatangaza ajira watendaji daftari wapiga kura

Spread the love  TUME Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), imetangaza nafasi...

Habari za SiasaTangulizi

Chadema yatangaza ruti awamu ya pili maandamano

Spread the love  CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema awamu ya...

Habari za Siasa

CCM yamkana mwenyekiti UVCCM aliyetaka wapinzani wapotezwe

Spread the love  CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimejitenga na kauli ya mwenyekiti...

Habari za SiasaTangulizi

Rais Samia kutunukiwa udaktari wa heshima Uturuki

Spread the loveBaraza la Chuo Kikuu cha Ankara, ambacho ni cha pili...

error: Content is protected !!