CHAMA cha Wananchi (CUF) kimepata pigo kwa kuondokewa na Muasisi wake, Mzee James Mapalala, aliyefariki dunia leo tarehe 23 Oktoba 2019. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Mzee Mapalala amefariki dunia katika Hospitali ya Kairuki, jijini Dar es Dar es Salaam, alikokuwa anapatiwa matibabu.
Maalim Seif Shariff Hamad, aliyekuwa Katibu Mkuu wa CUF, ameungana na Profesa Ibrahim Lipumba, Mwenyekiti wa chama hicho taifa, kuomboleza kifo cha Mzee Mapalala.
Kupitia ukurasa wake wa Twitter, Maalim Seif amesema amepokea kwa masikitiko kifo cha muasisi huyo wa CUF.
Maalim Seif amesema, Mzee Mapalala atakumbukwa kwa mchango wake alioutoa enzi za uhai wake, katika kupigania mageuzi ya kisiasa hapa nchini.
“Nimepokea kwa masikitiko taarifa za kifo cha Mzee James Kabalo Mapalala, aliyekuwa Mwenyekiti wa mwanzo wa CUF, kilichotokea leo Hospitali ya Kairuki, jijini Dar es Salaam. Mzee Mapalala atakumbukwa kwa mchango wake mkubwa katika kupigania mageuzi ya kisiasa hapa nchini,” ameandika Maalim Seif.
Wakati huo huo, Prof. Lipumba amesema CUF imepata pigo kwa kuondokewa na Mzee Mapalala, na kueleza kwamba, chama hicho kitaukumbuka mchango wake, hasa katika kuimarisha demokrasia.
Prof. Lipumba amesema, kwa kuthamini mchango wa Mzee Mapalala, CUF itasimamisha bendera zake nusu mringoti nchi nzima, hadi pale mwilo wake utakapozikwa.
“Tumepata taarifa za msiba, taratibu za mazishi hatujapata kwa ukamilifu lakini tutashiriki mazishi yake kwa kuuthamini mchango wake. Natoa agizo nchi nzima kuweka bendera nusu mringoti mpaka siku ya mazishi. Hii ni kuuenzi mchango wake,” amesema Prof. Lipumba.
Prof. Lipumba amesema Mzee Mapalala ni miongoni mwa waasisi wa chama hicho, ambaye alikijenga enzi za uhai wake. Na kufanikiwa kuweka mizizi ya chama hicho Visiwani Zanzibar na Tanzania Bara.
Leave a comment