KAMATI ya Uongozi ya Chama cha Wananchi ‘CUF’ imemtaka Kamishna wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Simon Sirro kuchukua hatua dhidi ya waliotekeleza uvamizi wa mkutano wa chama hicho mwishoni mwa wiki iliyopita, anaandika Hamisi Mguta.
Mkutano huo uliofanyika juzi na Mwenyekiti wa wilaya ya Kinondoni akiwa na waandishi wa habari kuzungumzia masuala mbalimbali ya chama hiko katika hoteli ya Vina iliyoko Mabibo uliingiliwa na watu waliovalia soksi usoni wakiwa na silaha za moto na marungu.
Akizungumza na waandishi wa Habari akiambatana na wajumbe wa kamati hiyo muda mfupi baada ya kukutana na Kamishna Sirro, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Julius Mtatiro amesema uamuzi huo ni baada ya kuona Jeshi la Polisi limekuwa kimya baada ya tukio la uvamizi huo kutokea.
“Tunaona hali inakoelekea ni mbaya na sisi wenye wanachama wengi tunashindwa kuwadhibiti watu wetu ikiwa polisi hawatawashughulikia wanaofanya matukio haya,” amesema Mtatiro.
Ameeleza kuwa ni mara ya 13 kutokea kwa matukio hayo na wamemuonya na kumomba asimamie polisi kufanya kazi yao katika tukio lililotokea Mabibo pamoja na matukio mengine yaliyopita.
“Hatutaki kuona nchi yetu inageuzwa kuwa sehemu ya umwagaji wa damu, hatutaki matukio ya watu kuuwawa yaanze kulipotiwa,” amesema.
Leave a comment