WAKATI uchaguzi wa Serikali za Mitaa ukiendelea kukaribia mwakani, Chama cha Wananchi (CUF) kambi ya Prof. Ibrahim Lipumba imeeleza kuwa, ‘atakaye ajiunge nao.’ Anaandika Yusuph Katimba … (endelea).
Abdul Kambaya, Ofisa Habari na Mawasiliano ya Umma CUF kambi ya Prof. Lipumba ambaye ni mwenyekiti wa chama hicho amesema, wao wanasonga mbele na mikakati ya kusuka chama hicho upya na kwamba hakuna anayesubiriwa.
Kambaya alikuwa akijibu swali la mwandishi alipotaka kujua kama kuna juhudi zozote zinazofanywa na chama hicho ili kumaliza mgogoro unaoendelea katika chama hicho na kusababisha kazi zake kudorora.
“Hakuna juhudi zozote zinazofanywa kwa sasa, zingekuwepo ningejua,” anasema Kambaya na kuongeza:
“Chama kinaendelea na taratibu zake, hakijamkataa mtu na anayetaka kuungana nasi aje.”
Kiongozi huyo ameeleza kuwa, utaratibu wa chama hicho upo wazi kwamba kila kinachofanywa kinazingatia matakwa ya katiba yao.
“Chama hiki kinahitaji kuwa imara, uimara wake unategemea uongozi na wanachama hivyo kinahitaji kuendelea kukikota kwa wanachama ili kiendelelee kuwa imara,” amesema.
Chama hicho cha upinzani cha tatu kwa ukubwa Tanzania Bara na cha pili kwa Tanzania Visiwani, kilitumbukia kwenye mgogoro mkubwa mwaka jana.
Ni baada ya Prof. Lipumba kuandika barua ya kujiuzulu uenyekiti wa chama hicho Agosti mwaka 2016 na mwaka jana kuandika barua ya kutengua barua yake ya kujiuzulu.
Hatua hiyo iliibua mgogoro wa kiuongozi baada ya kuibuka kwa pande mbili, mmoja ikipinga kurejea kwake na nyingine kubarika kurejea kwake.
Kwa sasa Prof. Lipumba anatambuliwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa kama mwenyekiti wa CUF.
Maalim Seif Sharif Hamad, Katibu Mkuu wa CUF ni miongoni mwa wasiokubaliana na uamuzi wa Prof. Lipumba kurejea kwa kuwa, aliomba kutojiuzulu lakini alifanya hivyo bila kulazimishwa na yoyote.
Mzozo huo umeongeza changamoto katika kutekeleza majukumu ya shughuli za chama hicho.
Leave a comment