BODI ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko (CPB), imesema ina mpango wa kuanza kutumia teknolojia ya kuzalisha mafuta ya kupikia yatokanayo na pumba za mpunga.
Uzalishaji huo unatarajiwa kuanza hivi karibuni kupitia kiwanda chake cha Mkuyu kilichopo jijini Mwanza. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma…. (endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dodoma leo tarehe 25 Oktoba, 2022 Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko (CPB), Dk. Anselm Moshi amesema sasa wapo katika upembuzi yakinifu katika kuongeza thamani mazao ya mpunga ili kuweza kuzalisha mafuta yatokanayo na pumba za mpunga.
Aidha, Dk. Anselm amesema bodi hiyo ya nafaka na mazao mchanganyiko ina mpango wa kuzalisha kuni kupitia pumba za mpunga katika kupunguza uharibifu wa mazingira.
Dk. Anselm amesema kwa mwaka 2021 taasisi hiyo imefanikiwa kununua mazao tani 64,000.
“Ikumbukwe kuwa Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko (CPB), ni Taasisi ya serikali chini ya wizara ya Kilimo iliyopewa dhamana ya kufanya biashara ya nafaka na mazao mchanganyiko na imeanzishwa kwa sheria ya nafaka na mazao changanyiko Namba 19 ambapo pia hadi sasa mzunguko wa biashara katika taasisi hiyo umeongezeka kutoka bilioni 15 hadi bilioni 52” ameeleza.
Leave a comment