Friday , 19 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa COVID-19: Serikali ‘hatuwezi kuepuka’
Habari za Siasa

COVID-19: Serikali ‘hatuwezi kuepuka’

Dk. Hassan Abbas, Katibu Mkuu wizara ya Habari
Spread the love

 

SERIKALI imeeleza kwamba, kutokana na muingiliano na mataifa mengine duniani, haiwezi kuepuka tahadhari juu ya maambukizi ya virusi vya corona (COVID-19). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).

Akizungumza na wanahabari leo tarehe 31 Januari 2021, kuhusu ziara ya Rais John Magufuli Kanda ya Ziwa, Msemaji wa Serikali, Dk. Hassan Abbas amesema, pamoja na muingiliano huo, watu wasitishwe.

“…kwa sababu ya muingiliano kati ya sisi na dunia, hatuwezi kuepuka kuendelea kuchukua tahadhari. Kwa hiyo Watanzania waendelee kuchukua tahadhari lakini tusiwe na woga wala tusichomekewe mawazo na mikakati ya watu wengine.

“Kuna watu wanatamani tujifungie ndani, sisi hatutafunga. shughuli zote ziendelee kama kawaida. Mambo ya michezo, mambo ya burudani, mambo ya shambani, mambo ya ofisini watu waendelee na shughuli zao kama kawaida, panapobidi kuchukua tahadhari, tuchukue tahadhari,” amesema Dk. Abbas.

Dk. Abbas ametoa kauli hiyo huku kukiwa na mvumo wa Kanisa Katoliki na Kanisa la Kiinjili Kilutheria Tanzania (KKKT) na wanasiasa wakiwatakawananchi kuchukua tahadhari zaidi na kwamba, ugonjwa huo kwa sasa ni tishio.

Hivi karibuni ni Yuda Thaddaeus Ruwa’ichi, Askofu Mkuu Mwandamizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, alitoa maagizo kwa waumini wao, kungeza tahadhari dhidi ya ugonjwa huo.

“Tusali na tujiombee sisi wenyewe, atulinde na janga la COVID-19. Hapa niseme kwamba COVID haijaisha, ipo kwa hiyo tusiende holela, tuwe makini na tujilinde,” alisema Askofu Ruwa’ichi katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Kumbukumbu ya Wafia Dini katika Kituo cha Hija Pungu, jijini Dar es Salaam.

Alisema “utamaduni wa barakoa tuliouacha wote, tuurudie tena, tujijali, tujipende, tujitunze, tushirikiane na Mungu katika kujilinda na tuendelee kuomba ulinzi kwa ajili yetu sote.”

Isaac Aman, Askofu wa Jimbo Kuu Katoliki la Arusha wiki iliyopita, alitoa waraka kwa kanisa hilo akiwataka waumini wake kutomjaribu Mungu kwa kupuuza kujikinga na maambukizi ya virusi hivyo.

“…tusimjaribu Mungu kwa kufanya uzembe na maisha yetu. Turejee tahadhari za kuzuia maambukizi bila ya kuwa na hofu,” aliandika Askofu Issac kwenye waraka wake aliotaka usomwe kwenye makanisa hayo Jumapili ya tarehe 24 Januari 2021. Waraka huo aliupa jina la ‘Kutembea Pekupeku Juu ya Mbigili.’

Jumanne ya tarehe 26 Januari 2021, Askofu Gervas Nyaisonga ambaye ni Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), aliwaandikia barua Mwadhama, Mpelekwa wa Baba Mtakatifu, Maaskofu Wakuu, Maaskofu na Maaskofu Wastaafu akiwataka kuchukua tahadhari ya maambukizi mapya ya corona.

“kwa uhalisia huo, tusiache kuwashauri, kuwahimiza na kuwaongoza Taifa la Mungu katika mapambano haya dhidi ya virusi vya corona,” aliandika.

James Mbatia, Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi, ameshauri wananchi kuchukua tahadhari ya maambukizi ya virusi vya corona, kwa kuwa ugonjwa huo upo.

“Taarifa za kidunia zinaonyesha, virusi vipya vya ugonjwa huu wa corona kutoka Afrika Kusini, Brazil na Ulaya vipo na maambukizi yake yameongezeka kutoka asilimia 30 mpaka 70, hivyo hatuna budi kujingika kwa kila Mtanzania,” amesema Mbatia na kuongeza:

“Ni wajibu wetu sote kulinda uhai wetu kwa gharama yoyote kwa kuwa ni janga la kidunia, tuondoke gizani kwa kila mtu kuchukua tahadhari kwa kuwa kila mtu ana haki ya kuishi…, suala la uhai ni jambo la mtu binafsi, hatuhitaji kibari cha serikali katika kujilinda kwenye jambo hili.”

Akiwa ziarani Kanda ya Ziwa, Rais Magufuli aliwataka Watanzania wasitishwe kuhusu taarifa za ugonjwa huo na kwamba, wasimame imara.

“Mtatishwa sana, ndugu zangu Watanzania lakini simameni imara. Ninajua wapo baadhi ya Watanzania hata wameondoka ndani ya nchi na kukimbilia maeneo mengine kwenda kuchanjwa, walipochanjwa huku walikuja kutuletea corona ambayo ni ya ajabu ajabu, simameni imara,” alisema Rais Magufuli.

1 Comment

  • Dak Abasi, tahadhali unayosema ni ipi? Kunawa mikono? Kuvaa barakoa? Kuepuka msongamano? Kupima? Chanjo? Tuwe wakweli
    Mnasema chanjo hatutaki kwa sababu ni ya wazungu. China na India zinasaidia hata Ulaya. Wao pia ni wazungu na mabeberu?
    Kama ni wazungu mbona chanjo za BCG, polio, diptheria, pepo bunda na kadhalika tunapokea kutoka kwa wazungu? Mbona marehemu Mwalimu Nyerere na Mkapa walitibiwa na wazungu huko Ulaya? Tusifichane
    Maaskofu wamesema. Je na masheshe na mufti mbona kimya?

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za SiasaTangulizi

Tanzania, Uturuki zanuia kukuza biashara, uwekezaji

Spread the loveSERIKALI za Tanzania na Uturuki zimekubaliana kuendeleza dhamira ya kuimarisha...

Habari za Siasa

Tume huru ya uchaguzi yatangaza ajira watendaji daftari wapiga kura

Spread the love  TUME Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), imetangaza nafasi...

Habari za SiasaTangulizi

Chadema yatangaza ruti awamu ya pili maandamano

Spread the love  CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema awamu ya...

Habari za Siasa

CCM yamkana mwenyekiti UVCCM aliyetaka wapinzani wapotezwe

Spread the love  CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimejitenga na kauli ya mwenyekiti...

error: Content is protected !!