GONJWA hatari la Corona, sasa limerejea kwa kasi katika Bara la Afrika, ambako mamilioni ya watu tayari wameambukizwa ugonjwa huo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Wimbi hili la pili la Corona linalokumba Afrika ni “kali zaidi” kuliko la kwanza, kwa mujibu wa Dk. John Nkengasong wa Kituo cha kudhibiti na kuzuia magonjwa Afrika (CDC).
Nkengasong ameliambia shirika la habari la BBC kwamba, bara hilo kwa sasa, linaripoti maambukizi mapya ya karibu 30,000 kila siku ikilinganishwa na 18,000 katikati ya mwezi Julai.
Takwimu za shirika hilo la afya zinaonesha kwamba Afrika kufikia sasa imethibitisha kuwa watu karibu milioni 3 wameambukizwa virusi vya corona, na vifo 68,755.
Nchi kama Rwanda, Namibia, Zimbabwe na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo zimeweka vikwazo vipya vya kuzuia kuenea kwa virusi.
Dk. Nkengasong alisema kuvaa barakoa ndio njia pekee ya kuzuia kuenea kwa virusi na kutoa wito kwa serikali kupunguza bei ya bidhaa hiyo.
Aliongeza kusema: “Unapotembea katika nchi tofauti barani Afrika inasikitisha kuona watu wengi hawavai barakoa mara kwa mara ama hawavai kabisa, na pia hawazingatii umati kati ya mtu moja na mwingine. Hii ni hatari, wimbi la pili ni kali sana.”
Leave a comment