JAIR Bolsonaro, Rais wa Brazil amewaambia wananchi wake, kwamba anaendelea vizuri ikiwa ni siku chache baada ya kutangaza kuambukizwa virusi vya corona (COVID-19). Inaripoti mitandao ya kimataifa…(endelea).
Jumanne wiki hii baada ya kufanyiwa vipimo, Bolsonaro alitangaza kwamba amebainika kuwa na virusi vya corona. Na kwamba, aliamua kufanya vipimo kwa kuwa alikuwa na joto kali pamoja na kikohozi.
“Nipo vizuri” Bolsonaro ameandika ujumbe huo kwenye ukurasa wake wa Facebook akisisitiza kwamba, amekuwa akitumia dawa aina ya Chloroquine ambayo haijathibitishwa na wanasayansi.
Matumizi ya Chloroquine katika kupambana na COVID-19, yaliyoanza kupigiwa chapuo na Donald Trump, Rais wa Marekani na baadaye Bolsonaro, yanapingwa na Shirika la Afya Duniani (WHO), kwamba hakuna ushahidi kuwa dawa hiyo inaponesha.
Katika Jiji la Hong Kong, China hali ya maambukizi ya COVID-19 inatishia amani ambapo serikali ya jiji hilo, imetangaza kufunga shule zote.
Maambukizi mapya 42 yaliyoripotiwa kwenye jiji hilo Jumanne wiki hii, imesukuma utawala kufunga shule hizo ili kuzuia maambukizi zaidi. Shule hizo zimetakiwa kufungwa kuanzia Jumatatu wiki ijayo.
Leave a comment